MTANZANIA una haki ya wewe kuwa na mwakilishi katika chombo kitakachozungumzia na kisha kusaidia kazi ya kuandika katiba mpya. Katika wakati huu, wewe mwananchi, raia wa Tanzania unapanda cheo na kuwa ndiye mwajiri wa rais,makamu wa rais, mawaziri, wabunge na watumishi wote wa serikali. Kazi yangu katika mchakato huu ni kuwaambia viongozi hao kwamba: 'tunawataka mtutawale hivi na uwezo na sifa zenu ziwe hivi. Kinyume cha hivyo tutawafuta kazi..' endelea kurasa inayofuatia:
Sunday, February 17, 2013
UTENZI WA K ATIBA MPYA 001-200
UTENZI WAKATIBA MPYA TANZANIA
UKMT 001-200
Utangulizi
Awali namshukuru,
Kunifanya mtu huru,
NIsiuzwe kwa ndururu,
Mtumwa nikabakia.
Namshukuru Rahimu,
Kwa kunigea kalamu,
Akanipa ualimu,
Maisha kuyaelewa.
Namshukuru Ghafuru,
Kwa kutonipa uzuru,
Katiba yetu kuzuru,
Na mimi kuibadili.
Utenzi nauandika,
Ili yangu kusikika,
Katiba ninayotaka,
Na ninayoitarajia.
Iwe inaeleweka,
Hakuna niliposhika,
Wala kundini kuwekwa,
Ila nilipoanzia.
Katikati nabakia,
Kwa yafaayo Tanzania,
Upande kutoegemea,
Ila kwa wasionielewa.
1.
WAKATI huwa wafika,
Watu wakaerevuka,
Wakahoji mamlaka,
Kwa vitendo na tabia.
2.
Mamlaka huwekeka,
Kwa chama kuchagulika,
Katiba inavyotaka,
Mshindi akatawala.
3.
Ila bado mamlaka,
Wananchi watayashika,
Kwa wao hukopesheka,
Ili kazi kuifanza.
4.
Huwa yote madaraka,
Watawaliwa washika,
Na muda wanapotaka,
Walioko huondoa.
5.
Katiba inayofaa,
Na dira itaanzia,
Ikaichora ruia,
Wapi tunaelekea.
6.
Njia tukishaamua,
Rahisi kuifatia,
Tasihili kuingia,
Haraka yakafanzika.
7.
Tunataka Tanzania,
Afrika ya kung'aa,
Isiyonayo udhia,
Kwingine tunaojionea.
8.
Umoja kuzungumzia,
Wote tukakubalia,
Vipi inavyotakiwa,
Nchi kuisimamia.
9.
Na tunaowachagua,
Vibarua kujijua,
Kazi wakiichezea,
Wajue twawatimua.
10.
Kanuni wakifulia,
Na sheria kuchezea,
Kortini wataingia,
Na kinga kuondolewa.
11.
Tunataka Tanzania,
Ya uchumi wa kukua,
Serikali nyenzo kuwa,
Ili watu kwendelea.
12.
Kikwazo inapokuwa,
Lazima kuondolewa,
Pasina ya kungojea,
Miaka wanayopewa.
13.
Kura wataitishia,
Ya imani kuridhia,
Watu wakiikataa,
Joho letu kulivua.
14.
Tunataka Tanzania,
Itakayotujalia,
Kila koo kupatiwa,
Nyumba bora ilokuwa.
15.
Vijijini kuanzia,
Kunakonukia balaa,
Watu wanakougua,
Kwa manyata kukalia.
16.
Tunataka Tanzania,
Hifadhi inayojua,
Ikazitunga sheria,
Ufujaji kukataa.
17.
Mahaini watakuwa,
Hifadhi wanaochezea,
Wakasagwa na kupewa,
Kazii kwenda tumikia.
18.
Tunataka Tanzania,
Maji isiyoishiwa,
Yakatiririka mwaa,
Kila nyumba kuingia.
19.
Tunataka Tanzania,
Ya umeme kusambaa,
Kila kaya kupatiwa,
Isiwe kwetu sanaa.
20.
Tunataka Tanzania,
Mazingira kuenziwa,
Mbadala kutumia,
Kwazo kuni na mkaa.
21.
Gasi tunayochimbua,
Mitaroni ikatiwa,
Kwenye nyumba kuingia,
Mjini na vijijini pia.
22.
Tunataka Tanzania,
Inayotujali afya,
Gharama kusaidiwa,
Utotoni kuanzia.
23.
Gharama zikaachiwa,
Ngumu zisizowawia,
Maskini Tanzania,
Nao wakajisikia.
24.
Mifuko iliyokuwa,
Utashi kuongezewa,
Siasa kuondolewa,
Uyakini kuwaniwa.
25.
Kiukweli watakiwa,
Huduma zao kutoa,
Wasiifanye nazaa,
Wakaja kuwa udhia.
26.
Mfano uwe Ulaya,
Uingereza kwangalia,
Mfuko uliotulia,
Huduma unazitoa.
27.
Wazee kuangaliwa,
Lazima kuwatajia,
Pasipo hilo kutiwa,
Tutakuja kulaniwa.
28.
Si wachache kwangaliwa,
Wengine kusahauliwa,
Kusutwa kukafatia,
Aibu tukaingia.
29.
Mzee ahitajia,
Umma kumuangalia,
Pasina kupendelea,
Cheo alichojaliwa.
30.
Wote sawa tuakuwa,
Kikatiba kwangaliwa,
Hili tukilifikia,
Nchi pepo itakuwa.
31.
Hili nalipigania.
Kwani nami najongea,
Nani ataniangalia,
Kama sio Tanzania?
32.
Madhumuni nayo nia,
Kuijenga Tanzania,
Karne ikatimia,
Bila cha kuongezea.
33.
Mfano yetu ikawa,
Katiba kwenye dunia,
Hadi nje ikang'aa,
Wakadhania ni jua.
34.
Sayari nyingine pia,
Na sisi zikavutiwa,
Huko wanakotokea,
Wakafata Tanzania.
35.
Vizuri tulianzia,
Mwalimu kutuongoa,
Umoja ukaenea,
Na amani kuivua.
36.
Nyuma waliofatia,
Mwinyi alijisemea,
Vichuguu tutakuwa,
Au sivyo ilivyokuwa ?
37.
Zimepishana tabia,
Uwezo umefifia,
Mfano aliyekuwa,
Laiki hajatokea.
38.
Enziye waliokuwa,
Mie wote nahofia,
Kama ningelijaliwa,
Cheo ningewazuia.
39.
Kwa mapambo wanafaa,
Si vitendo kuvijua,
Hawanayo nadharia,
Fedha waabudu sana.
40.
Wameshindwa kujijua,
Moja kubwa kuchagua,
Nafasi wanayopewa,
Mengi budi kuachia.
41.
Mlobaki nawambia,
Hili mkilitambua,
Uongozi ni ridhaa,
Wafaa kuheshimiwa.
42.
Na anayeulilia,
Budi kujipambanua,
Sio kwa kuumbilia,
Ila haki kutambua!
43.
Haya atakayezua,
Ubora atajaliwa,
Chini akatuondoa,
Hadi juu kufikia.
44.
Wengine tukiachia,
Tunaenda kufulia,
Hata tulichojaliwa,
Kitakuja kupotea!
45.
Ila hapa Afrika,
Mtindo umeshazuka,
Watawala wanataka,
Kuyatwaa mamlaka.
46.
Kutawala wanataka,
Si uongozi kuwika,
Hata kama wamechoka,
Nafasi huililia.
47.
Ndio maana twataka,
Katiba inayotamka,
Waziwazi kuyaweka,
Mianya ikaondoa.
48.
Hali yao kuijua,
Toka walipotokea,
Wafika ipi hatua,
Na kama wanaridhia.
49.
Kipimo wakikijua,
Na majibu kutambua,
Maamuzi huamua,
Mikakati kuibua.
50.
Mkataba kwangaliwa,
Hilo mojawapo huwa,
Wakafanya kurejea,
Upya ukapitiwa.
51.
Mazingira wakijua,
Si zamani yalokuwa,
Ndipo wanapomua,
Watu waweza kataa!
52.
Ukisoma historia,
Kasoro utaijua,
Katiba ya Tanzania,
Ya wananchi haijawa.
53.
Mkoloni katwachia,
Na yake aliyotia,
Vyake akajilindia,
Sio sisi kutufaa!
54.
Vingi ukiviangalia,
Ukoloni vyanukia,
Ila juu walokuwa,
Harufu haisumbui ?
55.
La hasha, ninakataa,
Vizuri waisikia,
Ila kinachotokea,
Harufu waizoea.
56.
Utamu unakolea,
Ubwana kuutumia,
Hivyo wakiviondoa,
Kawaida watakuwa.
57.
Hali juu watakiwa,
Ya wananchi wao kuwa,
Bila ya kuzingatia,
Katiba waikosea!
58.
Katiba waikosea,
Pamwe kupu'za sheria,
Mengi tunayatambua,
Wananchi wadhulumiwa.
59.
Wananchi wadhulumiwa,
Wao juu kutokuwa,
Watumwa si 'tumikiwa,
Wakuwa kuwalimia!
60.
Katiba yajitambua,
Sio juu walokuwa,
Wananchi kusimamia,
Wao ndio watakiwa!
61.
Vingine haya yakiwa,
Uporaji watokea,
Ni mkubwa uharamia,
Jinai tupu ikawa.
62.
Wakati wa Ujamaa,
Mengi yalifanania,
Mabnepari Tanzania,
Hali nyuma ya pazi!
63.
Ubepari kuingia,
Na ujamaa kuvia,
Hali mpya twazua,
Twatakiwa kulijua!
64.
Chama kilichoyatia,
Yatakiwa ondolewa,
Umoja wingi ukawa,
Na usawa kutetea!
65.
Ukabila wa kichama
Siasa sasa zafuma,
Ni balaa si neema,
Ila hatujalijua.
66.
Haki kuipigania,
Sasa lengo latakiwa,
Za halali kutumia,
Tenzi za demokrasia!
67.
Ni adui atakuwa,
Muua demokrasia,
Popote anapokuwa,
Lazima kumuondoa!
68.
Tunaitaka ruia,
Au visheni kujua,
Ni ramani inakuwa,
Mlango wa kujipitia.
69.
Budi hapa kuamua,
Kama bepari tutakuwa,
Nguo zote kuzivua,
Tusibakie na haya.
70.
Au kidogo kutia,
Machache yakabakia,
Wenye utu kuridhia,
Ubepari-ujamaa!
71.
Kila kitu kukitwaa,
Ubepari Tanzania,
Nchi tutaizingua,
Mhemuko ikatiwa!
72.
Yapo yakuangalia,
Na kisha kuyachagua,
Yale yanayotufaa,
Vyema tukayatumia.
73.
Mathalani tunajua,
Uzalishaji unafaa,
Watu wetu kuachiwa,
Nchi itaendelea!
74.
Biashara ni balaa,
Ovyo tunapoachiwa,
Kuchuma hupigania,
Hata watu tukaua.
75.
Huduma zinatufaa,
Pia kuziangalia,
Za kibepari zikiwa,
Kuna watakaofulia.
76.
Sera ninayolilia,
Mchanganyiko ikawa,
Mengi inachanganyia,
Kila bora kuchukua.
77.
Mbali tungelianzia,
Viongozi kuchungua,
Wazazi waliokuwa,
Na kama wametimia.
78.
Haramu wakiingia,
Wataileta nazaa,
Watu wakatunyanyua,
Badala ya chini kukaa.
79.
Kiongozi Tanzania,
Awe na historia,
Si tu ya kupitia,
Kwenye chama cha siasa.
80.
Inatupasa kujua,
Kizazi kilikoanzia,
Ukoo yake tabia,
Nayo wazi pia kuwa.
81.
Kuna asili udhia,
Kwa vita zinazaliwa,
Hitler aliyekuwa,
Kama huko katokea.
82.
Utoto ulivyokuwa,
Wenzie akiwafanyia,
Kama babe lilikuwa,
Bado litaendelea.
83.
Wazazi twapasa pia,
Na wao kuwatambua,
Bishara yake tabia,
Ndiko inakoanzia.
84.
Na jirani kutwambia,
kama kweli ilikuwa,
Wako wengi wakuzua,
Senti wakishazipewa.
85.
Rais awa Tanzania,
Usafi anatakiwa,
Nyumbani akianzia,
Hadi kazini kwingia.
86.
Shuleni tukayajua,
Rekodi kutupatia,
Sifuri waliokuwa,
Tusije tukaridhia.
87.
Ujana tukachungua,
Jinsi alivyotumia,
Anasa aliyejaa,
Aweza akatulia ?
88.
Njia alizopitia,
Zote tupate kujua,
Salama zinapokuwa,
Hapo twaweza pumua.
89.
Fujo waliozoea,
Ukubwani hurejea,
Kama vichaa wakawa,
Matatani kututia.
90.
Wakati ukifikia,
Urais kugombea,
Ushauri nautoa,
Njia bora kutumia.
91.
Adili tungeanzia,
Mapema kujipandia,
Wote wamoja tukawa,
kwenye hili kuamua.
92.
Je, rais maridhia,
Ni yupi atayekuwa,
Wajaao ukichaa,
Kabla mwaka kwingia?
93.
Ovyo kujipayukia,
Wao kiguu na njia,
Watu wakatumia,
Promosheni kuzua?
94.
Au kimya wa kukaa,
Kazi wanajifanyia,
Pasina kupendelea,
Kwao walikozaliwa?
95.
Nyuma wasosukumiwa,
Na ajenda walojaa,
Wataka kumtumia,
Zaidi kufanikiwa?
96.
Nini amewafanyia,
Kwao anakotokea,
Si wa kuwakimbia,
Hadi mlo kurejea!
97.
Ajenda alyezua,
Kwao na kwa jirani pia,
Umoja wakaujua,
Na kuipiga hatua.
98.
Elimu waliyopewa,
Kisha wakaitumia,
Wakatunga nadharia,
Wengine kujisomea!
99.
Au waliofulia,
Katu wasiobukua,
Vijiwe wavikalia,
Wakaongeza ujuha?
100.
Kiakili kakomaa,
Na kazi anaijua,
Au yeye angojea,
Wengine kumfanzia?
101.
Awe anayeamua,
Pasina na kuchungua,
Au anayechimbua,
Kwa haki akaamua?
102.
Hasira anayejaa,
Ovyo kujitamkia,
Murua akapungua,
Na kasoro kumjaa?
103.
Au aliyetulia,
Tathmini aijua,
Achukuaye wasaa,
Kila kitu kupembua?
104.
Kwake anayetulia,
Sio kiguu na njia,
Yake yakitengemaa,
Ndio akajitokea?
105.
Nyuma asiyefatiwa,
Na hila waliojaa,
Nchi wakajiuzia,
Hali yeye asinzia?
106.
Anachukua wasaa,
Kujisomea sheria,
Japo amepotia,
Mbalimbali tasnia ?
107.
Katiba akaijua,
Kufumba na kufumbua,
Chenga kutoadhiriwa,
Kwani yote ayajua?
108.
Imani aliyejaa,
Si asiyejitambua,
Kama boya yeye kuwa,
Baharini aelea!
109.
Pande asiyeegemea,
Na mjini kazaliwa,
Huko kutopendelea,
Vijijini kuwafaa.
110.
Kabila alozaliwa,
Juu kutoinuliwa,
Kwa hasara ya jamia,
Ukiwa wakaingia.
111.
Dini asiyetumia,
Wala zisizomtumia,
Usawa kusimamia,
Mola akapendezewa!
112.
Uungu kutojitia,
Unyonge akauvaa,
Kisha akanyenyekea,
Hata wadogo wakiwa?
113.
Dola asiyetumia,
Watuwe ngeu kutia,
Na macho wakaugua,
Na viungo kulemaa.
114.
Askari kuwatumia,
Uhalifu kuzuia,
Sio kuwageuzia,
Mbwa walioibiwa!
115.
Rushwa asiyeachia,
Polisi kuwa hidaya,
Ikageuka kinyaa,
Na watu kuwachukiya.
116.
Mkuu anayejaliwa,
Polisi kumsikia,
Kisha wakamhofia,
Huruma asiyekuwa.
117.
Asiyependa udhia,
Na raia kupakaziwa,
Awezaye kupindua,
Kila kitu kipya kuwa.
118.
Mahakama mwenye nia,
Uhuru kuiachia,
Sio kuiingilia,
Yeye akajipendelea.
119.
Bunge la waheshimiwa,
Uhuru kuliachia,
Sio mbeleko kutiwa,
Wakawa waning'inia.
120.
Adili ninarejea,
Lazima kutangulia,
Hili sio la kwachia,
Muda ukayoyomea.
121.
Wapaswa Watanzania,
Ukweli kujivunia,
Uongo anayetumia,
Huyo tukamuumbua.
122.
Kama cheo alipewa,
Iwe budi kuachia,
Na vingine kuvuliwa,
Hadi uchi kubakia.
123.
Uwizi kwa Tanzania,
Waweza sana pungua,
Mfano juu kukiwa,
Cheoni kuondolewa.
124.
Hata wakisingiziwa,
Na uwizi kunukia,
Harufu itatufaa,
Mamlaka kuyatwaa.
125.
Ngono akishuhudiwa,
Mara moja kumwengua,
Kazi asijechafua,
Ya watu kuathiriwa?
126.
Mlevi hatatufaa,
Na uraibu wake pia,
Katu kutokaribia,
Ikulu kwenda kukaa.
127.
Kupimwa inatakiwa,
Akili tukazijua,
Wapo walio vichaa,
Tusije kuwaachia.
128.
Ovyo wanaokimbia,
Njiani kujiropokea,
Wasiwasi wanatia,
Kama hawajapungua.
129.
Kama hawajapungua,
Au hawajazidiwa,
Kushonana zimejaa,
Zinashindwa kupumua.
130.
Mheshimu familia,
Huyo ataka enziwa,
Na wana kumsaidia,
Watu wema kuja kuwa.
131.
Katiba inatakiwa,
Kwa ufupi kurejewa,
Ili yetu kuepua,
Yaliyoiva haswaa.
132.
Mifano tunaijua,
Huko Kenya na Zambia,
Zimbabwe wafatia,
Ghana tukamalizia.
133.
Mageuzi yatakiwa,
Wakati ukishawadia,
Mabadiliko kuzua,
Nchi yakaja okoa.
134.
Elimu kuinyanyua,
Daraja jipya ikawa,
Malengo tukayajua,
Na dira kufafanua.
135.
Uchumi ili kufaa,
Watakiwa kufuliwa,
Tayari ukishang'aa,
Njia sahihi kujua.
136.
Hamsini kutimia,
Ni aibu tena waa,
Umaskini kubakia,
Lazima kuondolewa.
137.
Ulaya wametangulia,
Amerika kufatia,
Uarabu wajitoa,
Na Asia wanakimbia.
138.
Afrika twabakia,
Indiketa kwangalia,
Sasa basi twaamua,
Lazima kujichochea.
139.
Tutumie kila njia,
Kwa katiba kuandaa,
Milango inayofungua,
Kuuondoa ufakiri.
140.
Ufakiri ni balaa,
Kwetu kutoruhusiwa,
Wapaswa kushambuliwa,
Bilkuli kuung'oa.
141.
Neema ikabakia,
Waafrika kujaliwa,
Tukaacha angaliwa,
Kama 'boi' tulokuwa.
142.
Heshima kujipatia,
Tuache kutegemea,
Yetu tukajifanzia,
Kwa akili kutumia.
143.
Rasilimali zajaa,
Hadi wanatuibia,
Laiti tukijijua,
Haya hayatatokea.
144.
Wataingia vichaa,
Vita kutuanzishia,
Kama ilivyokuwa,
Amerika Latinia.
145.
Na Vietnam pia,
Waasisi twawajua,
Ufaransa kaanzia,
Marekani kafatia.
146.
Vyema tukawaambaa,
Mchina kutusaidia,
Vitani kutoingia,
Kwa yasiyotusaidia.
147.
Mmarekani balaa,
Watu apenda tumia,
Na hapo usipomfaa,
Teke atakutupia.
146.
Dunia ya kuchagua,
Pande ipi kwegemea,
Zipo safi na balaa,
Yafaa kuzikimbia.
147.
Mugabe ametuusia,
Mashariki kwanglaia,
Rahisi tukavijua,
Na salama vilokuwa.
148.
Vinginevyo kuumia,
Kawaida itakuwa,
Pasiwe wa kumlilia,
Wala kupata fidia.
149.
Misingi inayotakiwa,
Uhuru kuutetea,
Kila mtu huru kuwa,
Pasina ya kudhulumiwa.
150.
Wito nawatangazia,
Wote wanaonisikia,
Taasisi kuvumbua,
Mafunzo bora kutoa.
151.
Ya mwalimu taasisi,
Iwe ndiyo muasisi,
Ikaanzia kwa kasi,
Insha zake kufunza.
152.
Za mwalimu nadharia,
Wana wakaandaliwa,
Mazuri wakayajua,
Na dhaifu kugundua.
153.
Ubepari twauvaa,
Ila twaona wapwaya,
Bado zeke nadharia,
Hazinaye kufichua.
154.
Mbio kutokimbilia,
Ubepari kutuoa,
Tutakuja lijutia,
Tukabakia wakiwa.
155.
Taratibu inafaa,
Mchanganyiko ukawa,
Ya mtu yasiyofaa,
Umma wote kuachiwa.
156.
Umma wasiyopembua,
Ukiritimba kujaa,
Hayo tukawaachia,
Binafsi kufanzia.
157.
Haki ikaangaliwa,
Kwa wote sawa ikawa,
Pasiwe wa kununua,
Wala wa kujiuzia.
158.
Usawa unatakiwa,
Wote tupate jaliwa,
Sio wakapendelewa,
Hao wanaowajua.
159.
Na sisi tukaonewa,
Pamwe na kusahauliwa,
Hadi tukajichukia,
Na kuibeza dunia.
160.
Wana tunaojizalia,
Tusije tukawagawa,
Wenyewe kujibagua,
Kikazuka kizaazaa.
161.
Nchi tukajijengea,
Kila mtu kuridhiwa,
Uhuru kutunukiwa,
Halali kujifanzia.
162.
Kama maua tukawa,
Kila aina twajaa,
Hali tofauti zawa,
Rangi tulizojaliwa.
163.
Sheria inatakiwa,
Juu ya wote ikawa,
Kwa rais na raia,
Hapo wote kuwa sawa.
166.
Zama zajiondokea,
Mkuu juu kwachiwa,
Yake akajifanzia,
Hata yaliyo udhia.
167.
Rais akiachiwa,
Akawa juu ya sheria,
Twaweza pata kichaa,
Kama Amin akawa.
168.
Ikulu wakaingia,
Kitu wasiosikia,
Wakilindwa na sheria,
Wengi tutagugumia.
169.
Mawaziri watakwea,
Kuta wasizopitia,
Kwa kuwa wajitanua,
Rais kawachagua.
170.
Makamanda nao pia,
Kiburi kitawajaa,
Kwani wamechaguliwa,
Na kiranja alokuwa.
171.
Kadhalika wa mikoa,
Jeuri watatumia,
Watu wakawaonea,
Na vituko kuvizua.
172.
Aidha kwenye wilaya,
Yao watashupalia,
Na huku wakijitia,
Juu inawatumia.
173.
Usawa unatakiwa,
Ikatawala sheria,
Kila mtu akijua,
Akikosa huumia.
174.
Pasiwe wa kuumia,
Na katu wasioumia,
Neema wanaopewa,
Na mkuu aliyekuwa.
175.
Haki kuipigania,
Katiba inatakiwa,
Asiwe wa kuminyiwa,
Na kisha akaonewa.
176.
Pasiwe wa kununua,
Kisha akajiuzia,
Twaona yanayotokea,
Uhasama yanazua.
177.
Kibao hugeuziwa,
Haki apaswaye pewa,
Mwenye fedha akitoa,
Yeye akazawadiwa.
178.
Hilo budi kukataa,
Lisiachwe kwendelea,
Itavia Tanzania,
Hadi vita kuingia.
179.
Haki anayechezea,
Katu kutovumiliwa,
Maporini kutupiwa,
Bure akatumikia.
180.
Kama vile Serbia,
Inavyofaa Russia,
Unakofichwa udhia,
Wananchi salama kuwa.
181.
Rais kaelemewa,
Mamlaka kuyagawa,
Hili jambo la kufaa,
Vikwazo tutaondoa.
182.
Mkuu akichagua,
Wa polisi alokuwa,
Hatotii Tanzania,
Yeye kumnyenyekea!
183.
Mawaziri watakiwa,
Kazi wakajiombea,
Wabunge wasiokuwa,
Ila sifa walokuwa.
184.
Hawa wakiendelea,
Majimbo mengi kupwaya,
Yatakayoendelea,
Na waziri yalokuwa.
185.
Na wakuu wa mkoa,
Hebu tuache hekaya,
Sasa tumeshafulia,
Kuchaguliwa ni njia.
186.
Kuchagulwa ni njia,
Si rais kuteua,
Watu wakatupatia,
Na uchungu wasokuwa.
187.
Vyama pia vyatakiwa,
Mikoa kuigombea,
Ushindani vikatia,
Ustawi ukakua.
188.
Ninatamani pia,
Kuwa bunge la mkoa,
Waziri likachagua,
Mkuu atakayekuwa.
189.
Mkoa huru ukiwa,
Nchi itachachamaa,
Ushindani ukakuwa,
Mikoa kujinyanyua.
190.
Ya Mtwara kutokea,
Ni vigumu itakuwa,
kwa kuwa yao wapewa,
Na vyetu watuwekea.
191.
Mabunge wayalilia,
Pengine kwa kutojua,
Mawili tu kupatiwa,
Mimii ninaongezea...
192.
Mabunge yanatakiwa,
Thelathini ya mkoa,
Kisha yakafatia,
Mawili ya kitaifa.
193.
Ya mkoa kuzungumzia,
Yanyohusu mkoa,
Bila muda kupotea,
Na porojo kuzagaa.
194.
Ya taifa yatakuwa,
Mawili yaliyoshupaa,
Moja la kuchaguliwa,
Pasina wa kuteuwa.
195.
La pili la kuteua,
Makundi kwenye jamaa,
Maslahi kufatia,
Kwa karibu na ridhaa.
196.
Ya mikoa kutumia,
Muda mwingi na wasaa,
Ya taifa kwa masaa,
Ya kwao yakatimia.
197.
Hapo tukishafikia,
Itafungka Tanzania,
Kutakwisha kutambaa,
Tukaanza kutembea.
198.
Hatua ikafatia,
Mbio tuanze tumia,
Maendeleo kuzua,
Ya kweli yatayokuwa.
199.
Mahakama inatakiwa,
Huru itakayokuwa,
Mtu asiyoingilia,
Akazipinda sheria.
200.
Jaji mkuu Tanzania,
Asiwe wa kuteua,
Wengi wangechaguliwa,
Bunge Jaji kumchagua.
UTENZI WA K ATIBA MPYA 201-400
UKMT 201-400
201.
Wakiona anafaa,
Tiki watampatia,
Na kisha kuwaachia,
Wajuzi kumhudumia.
202.
Hata rais akiwa,
Mahakama juu kuwa,
Yake atapitishia,
Tu yanakoruhusiwa.
203.
Yeye hatapendelewa,
Wala akaogopewa,
Bali itakapokuwa,
Hatari inahofiwa.
204.
Hatari kuamuliwa,
Watu wote kuzijua,
katibani kuainiwa,
Waziwazi tukajua.
205.
Vyombo vyetu vya habari,
Vinayo kubwa safari,
Hasa vyenye majemadari,
Siasa wanaobwia.
206.
Hivi vingelitakiwa,
Na baraza kwangaliwa,
Uovu kutambuliwa,
Na wema kuzawadiwa.
207.
Na wanaovitumia,
Kamasi kujifutia,
Katu kutokuachiwa,
Wala wakaruhusiwa.
208.
Ni nguzo ya kitaifa,
Haikubaliki nyufa,
Huo mbaya wadhifa,
Hatari unavutia.
209.
Ajira inatakiwa,
Vizuri kufunuliwa,
Na ujira kupatiwa,
Utumwa usiotia.
210.
Vingine ukiachiwa,
Wengi watanunuliwa,
Rushwa wasioijua,
Hapo kazi kupatiwa.
211.
Serikali yatakiwa,
Mwongozo kuridhia,
Taarifa kuzitoa,
Bila ya kulazimishwa.
212.
Mswaada unachelewa,
Ruhusa unaotoa,
Waandishi kuingia,
Taarifa kupakua.
213.
Siri budi kuzijua,
Zipi zinazostahilia,
Zingine nyingi balaa,
Wananchi zinatuibia.
214.
Hii yetu Tanzania,
Dini haikujaliwa,
Ila tuliozaliwa,
Zetu tumejirithia.
215.
Hivyo hatutoridhia,
Imani kuzichezea,
Dini wanaotambua,
Katiba ya Muumini.
216.
Matangazo ya zinaa,
Hapa kwetu Tanzania,
Kwanini yaruhusiwa,
Yaongeza umalaya.
217.
Kondomu yanasifia,
Na ngono kuichochea,
Na tunachojipandia,
Ni kukithiri ukiwa.
218.
Na utamu waitia,
Kwa ladha na kunukia,
Hii nikiangalia,
Naona chambo kinakuwa.
219.
Mila tungezirejea,
Kiini kukiagua,
Ya wazungu tukilea,
Tutakuja kujutia.
220.
Walau wanaonewa,
Kulia waliokuwa,
Kushoto wakidhania,
Ndio wanapendelewa.
221.
Redio wachakachua,
Na mitabendi kuvia,
Ruhusa waililia,
Tivii wakataliwa.
222.
Kiini hawajakijua,
Ila udini wahofia,
Haya tungeangalia,
Usawa ukaenea.
223.
Auaye kuuawa,
Vingine haitakuwa,
Amri tulikwishapewa,
Msije kuipindua.
224.
Hata na huko Ulaya,
Uhalali waujua,
Kifo anayekusudia,
Kifo malipo hupewa.
225.
Kadhi haiwi halali,
Kumfanyia udhalili,
Wapewao kulhali,
Huyu wakamkamia.
226.
Uhuru wa kuabudu,
Jumlaye maabadu,
Budi kutia hadidu,
Mahakama si ridhaa!
227.
Mahakama yatakiwa,
Islamu kuwafaa,
Kuwanyima ni hadaa,
Shere mnawachezea.
228.
Katiba inatakiwa,
Hili ikalitambua,
Na ujanja kuzuia,
Waumini kufanziwa.
229.
Yao wakiikataa,
Ya sekula kutumia,
Na zote zinatakiwa,
Dola kuziangalia.
230.
Ubaba wa kujitia,
Unatakiwa kujifia,
Hakuna wana wakawa,
Mbelekoni kwenda tiwa.
231.
Watu wetu wamekua,
Na uhuru kuchagua,
Lile wanaloamua,
Kwanza likafikiriwa.
232.
Ila waliojaliwa,
Kweli wakishatambua,
Halafu wakafichua,
Hiari budi ikawa.
233.
Wingi wetu kuutia,
Katibani kuridhiwa,
Vyana tumevizua,
Budi kuvihudumia.
234.
Vijijini watakiwa,
Uzuri kuelezewa,
Vyama vingi kujaliwa,
Neema tutajaliwa.
235.
Hivi vitapigania,
Lilo bora kupatiwa,
Mmoja wa kuchezewa,
Tena hatajabakia.
236.
Vyama pia vyatakiwa,
Ustawi kuchangia,
Miradi wakafungua,
Kujenga yetu mikoa.
237.
Na anayewazuia,
Upinzani Tanzania,
Huyo ni wetu adawa,
Anafaa kuchukiwa.
238.
Upinzani wafungua,
Vile tulivyofungiwa,
Uono ukautoa,
Mbali unaofikia.
239.
Vijijini ukikua,
Vijiji havitavia,
Na huko kwa kuanzia,
Haki kuzipigania.
240.
Haki kuzipigania,
Vijiji vikapatiwa,
Bora waliojaliwa,
Viongozi wa kufaa.
241.
Si bora wa kukaa,
Kitu wasiotambua,
Miaka ikaishia,
Vilevile kubakia.
242.
Uongozi ninalia,
Chini ndiko watakiwa,
Vijiji kuviinua,
Hadhi bora kufikiwa.
243.
Vijiji vinaumia,
Toka Nyerere kutwachia,
Nani wa kuangalia,
Isipokuwa Katiba.
244.
Iliyo yajisemea,
Uwiano utakuwa,
Katika kuendelea,
Ila mengine yafanzwa.
245.
Haki yaegemea,
Miji kuipendelea,
Huduma huko zajaa,
Vijijini ni adimu.
246.
Kikomo tungekitoa,
Vya msingi kupatiwa,
Hilo litachochea,
Vijiji kuvifufua.
247.
Maji tarehe tukawa,
Sote tunaitambua,
Huko yatawafikia,
Ima fa ima ikawa.
248.
Umeme aidha pia,
Tarehe tukaijua,
Gizani kuwaondoa,
Kushindwa kutokubali.
249.
Zahanati za kufaa,
Mwisho kuukadiria,
Kila kijiji pakawa,
Tiba nao wanapewa.
250.
Shule nazo tukajua,
Kila hali zatimia,
Pasina kitu kuvia,
Wala kikakosekana.
251.
Barabara nazo njia,
Mkakati kuufua,
Wanavijiji wakawa,
Wao waziangalia.
252.
Wao waziangalia,
Lakini tukalipia,
Vyanzo vikalelewa,
Endelevu hilo kuwa.
253.
Masoko kuwajengea,
Na hadhi yaliyokuwa,
Wao wakajikodia,
Maduhuli kuingia.
254.
Na uongozi kupatiwa,
Msasa unaotiwa,
Elimu wakagawiwa,
Ubora wao kukuwa.
255.
Maarifa kuletewa,
Ujasiriamali kwanzia,
Njia wakazing'amua,
Ufukara kuuvua.
256.
Huku juu wamejaa,
Hawana la kujifanyia,
Nafasi waitumia,
Kuutembeza umbeya.
257.
Na uongo kuzua,
Wengine kupakazia,
Wakubwa wasio haya,
Wamejaa Tanzania.
258.
Wanashindwa kutambua,
Siku itajaingia,
Mseto kuandaliwa,
Wapi watachungulia?
259.
Chama kimoja udhia,
Mengi kimetuulia,
Hesabu nikiitoa,
Mbona wengi mtalia.
260.
Ushirika kimeua,
Na kushindwa kufufua,
Nini wanajivunia,
Maiti kilichokuwa ?
261.
Vijiji vimechakaa,
Hoi taabani vyawa,
Wasichana angalia,
Wazee utadhania?
262.
Maji wanayfukua,
Sio ya kufungulia,
Maili wanatembea,
Porini kuyafatia.
263.
Na wengine wanaliwa,
Na wanyama wenye njaa,
Hakuna wa kutetea,
Hili mara moja lishe.
264.
Moto wanaotumia,
Kuni za kupigania,
Kisha wakachuchumaa,
Hadi kuwaka dunia.
265.
Macho yanaugulia,
Hadi mekundu yakawa,
Uzee ukiingia,
Uchawi wanazuliwa.
266.
Makampuni waua,
Na kisha kujinunulia,
Ufisadi unapwaya,
Chini wanazimwagia.
267.
Halmashauri zapwaya,
Imara zilizokuwa,
Siasa zilipoingia,
Hewa zikaichafua.
268.
Miundo inatakiwa,
Ya vyama vingi kuzua,
Inayoyachangamkia,
Chama inayoyachukia.
269.
Mifumo inatakiwa,
Kuzua teknolojia,
Haki ikatutendea,
Sisi sote Tanzania.
270.
Wanachama kuwajua,
Muhimu teknolojia,
Simu ukizitumia,
Idadi mtaitambua.
271.
Sio wanaoishiwa,
Mamluki kutumia,
Dodoma kupakuliwa,
Mizigo ukadhania.
272.
Simu mkizitumia,
Wafu wenu kupungua,
Hisabu ikatimia,
Michango kwa kuitoa.
273.
Wenye simu wanajua,
Orodha kuiandaa,
Ujumbe wakautia,
Ada kuikumbushia.
274.
Wanachama wakatoa,
Za kwao mkatumia,
Na sio kutupunguzia,
Kidogo kilichokuwa.
275.
Kama SACCOS kuundiwa,
Watu wanapochangia,
Mikopo wakaachiwa,
Pasina riba kutia.
276.
Wanachoma watatoa,
Ili mkopo kupewa,
Ubahili kupungua,
Na nyodo zikapotea.
277.
Biashara mtazua,
Nzuri na ya kusifiwa,
Wafuasi kunyanyua,
Na vyam mkaviokoa.
278.
Benk Kuu Tanzania,
Kuwa huru yatakiwa,
Ikaweza kuamua,
Pasina kuingiliwa.
279.
Gavana kwa kuanzia,
Lazima kuchaguliwa,
Jina bunge kupatiwa,
Pamoja kumridhia.
280.
Hesabu akitimia,
Kura apate pigiwa,
Akitoka kidedea,
Fursa akaachiwa.
281.
Aweza nje tokea,
Kama kazi aijua,
Si lazima kuchukua,
Mzawa alo mbaya.
282.
Ajira atazitoa,
Wasaidizi kuchagua,
Malengo kujiwekea,
Si vyama kutuambia!
283.
Siasa imechafua,
Benki Kuu Tanzania,
Ufisadi twaujua
Ndiko ulikoanzia.
284.
Vyama vinaivamia,
Na bakuli wachukua,
Msaada kulilia,
Kwa yao si Tanzania.
285.
Na wakuu twaambiwa,
Huko wanaogopewa,
Mikopo wakiamua,
Upesi waruhusiwa.
286.
Marufuku ingekuwa,
Benki kuikaribia,
Wanasiasa Tanzania,
Mbali sana wakakaa.
287.
Kisha benki yatakiwa,
Ubunifu kukazia,
Njia ikazigundua,
Ufakiri kuuvaa.
288.
Budi kujali mzawa,
Na yake kuyaangalia,
Kwa sera zinazofaa,
Kipato kutuongezea.
289.
Kuchangamsha yatakiwa,
Benki inazoangalia,
Ili kujititimua,
Mikakati kuzindua.
290.
Mikakati kuzindua,
Mikopo ikatolewa,
Na dhamana wakapewa,
Hasara kutoingia.
291.
Kichocheo yatakiwa,
Benki Kuu kwetu kuwa,
Si mzgo kuchukua,
Kitu usiotufaa.
292.
Mbele yatakiwa kuwa,
Benki Kuu Tanzania,
Dira ikaangalia,
Na udhibiti kupea.
293.
Vyama kutokutegmewa,
Kazi hii kuingilia,
Benki kuu yatimia,
Ndio itakayoamua.
294.
Rahisi kwetu ikawa,
Chama tunapochagua,
Na kingine kuondoa,
Bila hazina kuibiwa.
295.
Maadui Tanzania,
Upya inatakiwa,
Sasa hivi kuwajua,
Kwa maadili kuzua.
296.
Tunao tunaojua,
Hao wa kihistoria,
Toka uhuru kupewa,
Kuwepo waendelea.
297.
Umaskini Tanzania,
Mradi umeshakuwa,
Watu wanachachamaa,
Unafugwa na wakubwa.
298.
Unafugwa Tanzania,
Ufukara kuwafaa,
Viztio wasosha njaa,
Mitambi kuitambia.
299.
Kama wangeliamua,
Ni rahisi kuuzoa,
Mbali kuufagilia,
Kwa hivi tulivyojaliwa.
300.
Ila eti wahofia,
Huru watu watakuwa,
Njaa wakishaondoa,
Hawawezi chaguliwa.
301.
Umma budi kuamua,
Walo bora kuchagua,
Bila ya kufikiria,
Chama wanachotokea.
302.
Ujinga tunahofia,
Hivi sasa warejea,
Katiba inatakiwa,
Hili ipate zuia.
303.
Kwa kuagiza sheria,
Mfuko kuzinduliwa,
Utakaoangalia,
Ujinga kutokusambaa.
304.
Mikakati itazua,
Itakayotungwa sheria,
Na watu wa kubobea,
Na wengineo raia.
305.
Kitu kinachotakiwa,
Ujinga kutoruhusiwa,
Shule zikadhaminiwa,
Za msingi zilizokuwa.
306.
Kisha kasma kupewa,
Elimu kutofifia,
Watu wazima raia,
Wakawa wanajisomea.
307.
Jioni wataingia,
Kusoma wapate jua,
Aidha kuandika pia,
Ya msingi kuyajua.
308.
Kama vyuo vitakuwa,
Maarifa kufunziwa,
Yatayoamuliwa,
Na wao wenyewe raia.
309.
Na wao wenyewe raia,
Eneo wanalokaa,
Wakafunzwa kujifaa,
Umoja na kujitegemea.
310.
Maradhi yanakimbia,
Ila mapya yaingia,
Na kasi yaliyokuwa,
Na kuongeza tanzia.
311.
Mikakati yatakiwa,
Hasa tiba kuvumbua,
Gharama kutokupaa,
Huduma watu kukosa.
312.
Wengi wanazihofia,
Hospitali Tanzania,
Waganga waogopewa,
Sio tena kudekewa.
313.
Nashauri Tanzania,
Kazi hizi kwangalia,
Daktari juu kuwa,
Ujira wanaopewa.
314.
Na manesi nao pia,
Njaa kutowavamia,
Ikawa rushwa wapokea,
Ndio watoe huduma.
315.
Wao wakidhulumiwa,
Na sisi tutaonewa,
Vipi wasiotufaa,
Ndio zaidi walipwa ?
316.
Kuanzia sasa yafaa,
Watumishi kupatiwa,
Ajira kwa kuzingatia,
Elimu wlaiyofikia.
317.
Hata waziri akiwa,
Vyetiwe kuviangalia,
Na kisha kudadavua,
Majukumu ya kufaa.
318.
Uzito kuongezewa,
Kama zaidi kapewa,
Ila hatutarajia,
Viongozi juu kuwa.
319.
Juu wanaotakiwa,
Mishahara kuchukua,
Ni tabibu Tanzania,
Na wanaotuokoa.
320.
Utamu pakufikia,
Wajuzi juu wakiwa,
Kazi waliobobea,
Wazuao ufumbuzi.
321.
Sera za watu kupewa,
Naona twapendelea,
Jasho pasina kutoa,
Swahiba wanyanyukia.
322.
Magwiji wanatakiwa,
Kazi zao kusomea,
Na kisha wakazijua,
Juu ndio kufikia.
323.
Wanasiasa wazua,
Wao wakajichotea,
Hali ukiangalia,
Kipato watukatia.
324.
Juu wanaotakiwa,
Njia wanazogundua,
Hazina ikawa yajaa,
Wala sio kupungua.
325.
Utamu wa kusifiwa,
Vyeo hivi kutungua,
Chini wakajishukia,
Majina yakabakia.
326.
Shule waliokimbia,
Kipato kikarejewa,
Na waliojinuia,
Haki yao kupatiwa.
327.
Elimu inatakiwa,
Kuwa ndiyo yetu taa,
Wengi inavyofikia,
Likawa lazawadiwa.
328.
Hapo tukishaifkia,
Na vihiyo kuishia,
Nchi itajiumua,
Mbele ikatangulia.
329.
Ila wanaotumia,
Za kwao za kuzaliwa,
Mambo wakatufanzia,
Wafaa kufikiriwa.
330.
Juu wakitunyanyua,
Na shule hawakujua,
Bado hao maridhia,
Wapaswa kuzawadiwa.
331.
Elimu fanifu kuwa,
Matatizo kuondoa,
Kila mwenye hiyo dawa,
Yafaa kumpa hidaya.
332.
Na elimu walopewa,
Wakashindwa itumia,
Wakawa watuibia,
Yafaa kuwaumbua.
333.
Kila mmoja akajua,
Ienzicho Tanzania,
Ni utumishi kutoa,
Si sura na kushangilia.
334.
Shule zetu Tanzania,
Mizani inatakiwa,
Tathmini kufanzia,
Viwango vyake kujua.
335.
Kuna hadhi kuwekewa,
Daraja tukalijua,
Za umma na za raia,
Uwiano kukisia.
336.
Hali zikahakikiwa,
Inavyokuwa dunia,
Wadau wakiridhia,
Yao yakakubaliwa.
337.
Ada tunapoanzia,
Kiasi tukakijua,
Thamani kudadavua,
Kila mtu akajua.
338.
Elimu kutoachiwa,
Kama vile duka kuwa,
Ila huduma ikawa,
Tunayoitegemea.
339.
Chakula kufikiria,
Lishe bora ilokuwa,
Menu wakazipatiwa,
Vyuo, shule kutumia.
340.
Kiwango juu kikawa,
Chini kutoshushiwa,
Hali ikawavutia,
Wageni kuja kusoma.
341.
Viwanja vinatakiwa,
Vya michezo kujengewa,
Kimataifa vikawa,
Ikatujua dunia.
342.
Somo la kujitegemea,
Bado nalipigania,
Shuleni kwenda tolwea,
Malezi kusaidia.
343.
Walimu tunatakiwa,
Idadi wanayotakiwa,
kwa darasa kutopungua,
Na kwa shule kuwajua.
344.
Mazoezi yatakiwa,
Watoto kujifanyia,
Homuweki wakapewa,
Pasina ya kukosea.
345.
Udhibiti watakiwa,
Ubora kuangalia,
Na mitaala kunyoa,
Aali kikabakia.
346.
Yafaa kulingania,
Binafsi na jumuiya,
Watu wakatambua,
Kweli linalotokea.
347.
Binafsi tukitumia,
Si tajiri tumekuwa,
Kiwango waangalia,
Nafasi kushindania.
348.
Ya juu inapokuwa,
Wana kutowabagua,
Umma na binafsia,
Usawa wote kupewa.
349.
Sasa rushwa Tanzania,
Adui mkubwa kawa,
Vyama zinaipokea,
Achia wao raia.
350.
Kanuni zinatakiwa,
Adui kumshambulia,
Maana wanaomujua,
Wasema hawajamjua.
351.
Ufafanuzi walia,
Lazima wapate pewa,
Mimi sijawalewa,
Ila naona nazaa.
352.
Rushwa ninavyoijua,
Ni kitu chochote kutoa,
Utakacho ukapewa,
Hata haramu ikiwa.
353.
Dola ikishafulia,
Mangimeza kuitwaa,
Udhibiti ukavia,
Basi hapo hustawi.
354.
Polisi wa Tanzania,
Kwalo hili wasifiwa,
Trafiki wamejaa,
Vipi zavunjwa sheria?
355.
Nyama wanaonunua,
Mchana ukiingia,
Ukienda ulizia,
Ni nani utaambiwa.
356.
Daladala kwenye njia,
Bodaboda nazo pia,
Bajaji ndio balaa,
Wamiliki wamekuwa!
357.
Vipi zitaheshimiwa,
Za kwetu nchini sheria,
Hali wao wajijua,
Wameshajitapikia ?
358.
Ila wanaojijua,
Vishawishi huvitoa,
Na mianya kubomoa,
Nchi salama ikawa.
359.
Magari wakinunua,
Mafuta ni ya kununua,
Mtu gari hujaliwa,
Ila mafuta hanayo.
360.
Mifukoni yatokea,
Hifadhi isiyokuwa,
Hapo hukugeukia,
Mstaafu kuibiwa.
361.
Ufisadi nao pia,
Kwetu sasa adawa,
Nje wanatoroshea,
Uswizi kujifichia.
362.
Ukabila Tanzania,
Naona waja mpya,
Wa kichama ulokuwa,
Kimoja wapendelea.
363.
Chamani usipokuwa,
Ugumu mamboyo huwa,
Viwanja kwa kuanzia,
Na biashara kwingia.
364.
Wao wajipendelea,
Wengine wanaonewa,
Haki sasa walilia,
Nchi yetu kutawala.
365.
Haki zikinunuliwa,
Uadui tunazua,
Polisi kuangaliwa,
Kwenye hili wabobea.
366.
Mahakimu nao pia,
Na mtu wakitumiwa,
Haki kweli itakuwa,
Hapa kwetu Tanzania?
367.
Kuna adui tamaa,
Na uchu ulioingia,
Watu wajitangazia,
kama tiketi kupewa.
368.
Wengine wakanunua,
Matope kuwapakaa,
Wao bora kujitia,
Ilhali twawajua!
369.
Matajiri Tanzania,
Adui waweza kuwa,
Wakianza kuvamia,
Ya imani kubomoa.
370.
Kuna miko yatakiwa,
Kwenye vitu kununua,
Wakfu inapokuwa,
Mara mbili fikiria.
371.
Mizimu inasikia,
Kwa wale wasiojua,
Huja hapa kurejea,
Ya kwao kuangalia.
372.
Wakikuta chaibiwa,
Hasira huwaingia,
Ukabaki kujutia,
Ya nini ulizaliwa.
373.
Nyumba kutokujengewa,
Naona tunachukiwa,
Hali wengine wapewa,
Hali chini wazikosa.
374.
Au shere twachezewa,
Na juu waliokuwa,
Ili yao kuja kuwa,
Budi viotani twishi?
375.
Katiba ingeamua,
Haki kuitangazia,
Nyumba kwa kila familia,
Lazima tukajengewa.
376.
Cuba walijifanzia,
Mengine kushughulikia,
Tatizo wakaliondoa,
Maendeleo kuzua.
377.
Hapa kwetu Tanzania,
Mkakati watakiwa,
Ikapeana mikoa.
Ili nyumba kujengeka.
378.
Viwanda watavizua,
Na ajira kuzitoa,
Yataka kujipangia,
Wito moyoni ukawa.
379.
Pawe katika mkoa,
Kuna wilaya kadhaa,
Kazi wanajipangia,
Kilimo kutumikia.
380.
Mkoa mmoja ukawa,
Kwa hali unajigawa,
Nafaka wakazizaa
Na ya biashara pia.
381.
Baadhi wawe wavua,
Kwa mabwawa kuyazua,
Samaki wakajilimia,
Na uchumi ukakua.
382.
Mboga mboga zatakiwa,
Ikachaguliwa wilaya,
Kujakulisha mkoa,
Na nje kujiuzia.
383.
Ufugaji kwa maziwa,
Na nyama unatakiwa,
Proteni zatuishia,
Na akili kupungua!
384.
Kweli ukitembelea,
Vijiji vya Tanzania,
Vingine utagundua,
Wahitaji kidogo tu.
385.
Mkakati hivi kuwa,
Kama biashara yawa,
Haraka tukajifanyia,
Hamsini yasochukua.
386.
Wanaweza kujinoa,
Ufakiri kuutoa,
Daraja wakanyanyua,
Kama watu nao kuwa.
387.
Ila juu walokuwa,
Watakiwa jionea,
Visa wakavisikia,
Na tiba kuichangia.
388.
SACCOS zikazaliwa,
Za ujenzi Tanzania,
Huko ikaongezewa,
Na simu wasiotoa.
389.
Watu watazichangia,
Ili kufika hatua,
Mtu akajikopea,
Deni la nyumba kulipa.
390.
Itang'aa Tanzania,
Hata vijijini pia,
Watu tukawanyanyua,
Ngazi mpya kufikia.
391.
Uhuru twajivunia,
Wa bendera ulokuwa,
Misingi imetwekea,
Tunaweza kutumia.
392.
La muhimu kutanua,
Uhuru ukaenea,
Nafsi zikaridhiwa,
Na makundi kujaliwa.
393.
Tunayoyazungumzia,
Tukaona yanafaa,
Sababu sijaijua,
Kwanini kutotelezwa ?
394.
Mfano naulizia,
Tume huru ilokuwa,
kwanini tunakawia,
Na ukweli twaujua?
395.
Mipaka hadhi kutia,
Kama viwanja vikawa,
Ndege tunakopandia,
Na sisi kuheshimiwa.
396.
Mutukula na Namanga,
Tunduma ni kuengaenga,
Hadhi mbele ikasonga,
Raia kujivunia.
397.
Mipakani na Rwanda,
Burundi nako kuranda,
Watu wanapokwenda,
Udhia uwe muhali.
398.
Msumbiji na Zambia,
Malawi na huko pia,
Asafiri Mtanzania,
Hali salama akiwa.
399.
Hakuna kuendelea,
Bila kuwa na ubia,
Nasi wanaotufaa,
Jirani watuzungukao.
400.
Mipaka bora ikiwa,
Biashara kuinua,
Na uchumi hupanua,
Soko kubwa kufikia.
UTENZI WA KAITBA MPYA TANZANIA 401-600
UKMT 401-600
401.
Tuwe ni wa kuanzia,
Wala si wa kungojea,
Kama taa Tanzania,
Tuangaze yao njia.
402.
Tanzania mshumaa,
Jirani waangalia,
Kitu tukikianzia,
Fedha ndani tutatia.
403.
Bandari kuiokoa,
Vifisadi kuvitoa,
Aibu wanaotia,
Jirani wakatuchukia.
404.
Bandari salama kuwa,
Mfano wa kutambuliwa,
Nchi ikajivunia,
Afrika kufurahia.
405.
Yafaa kufatilia,
Kila siku, kila saa,
Maana tunapajua,
Huko wankotwibia.
406.
Sahani tukiandaa,
Watumishi kuingia,
Wote tukafurahia,
Ya ukweli kuyajua.
407.
Watumishi wasifiwa,
Na wema waliokuwa,
Ila mabosi udhia,
Njaa imewazidia.
408.
Ukweli watatoboa,
Chini wanaoumia,
Hadi nguo kuzivua,
Wakubwa uchi wakawa.
409.
Bandari ikishang'aa,
Itawaza Tanzania,
Mabilioni kutwaa,
Tena yasijepotea.
410.
Mikoa inatakiwa,
Uchumi kuangalia,
Uhuru ikipatiwa,
Ushindani watazua.
411.
Ushindani wakizua,
Mikoa haitafifia,
Yao watapigania,
Wajezuka kidedea.
412.
Nishani tukizitoa,
Ziwe zinashindaniwa,
kati ya yetu mikoa,
Nguvu itaziumua.
413.
Na ukuu wa mkoa,
Wakati unaishilia,
Sasa anatakiwa,
Waziri Mkuu Mkoa.
414.
Naye akasaidiwa,
Na bunge la wake mkoa,
Ujerumani wajua,
Walioitembelea!
418.
Mawaziri huchagua,
Mkoa kujijengea,
Uchumi pia jamaa,
Wao wakaangalia.
419.
Serikali nchi kuwa,
Ulinzi yaangalia,
Na usalama kulea,
Kitaifa inafaa.
420.
Serikali bora kuwa,
Fedha inasimamia,
Kasma yake kutwaa,
Na wengine kuachiwa.
421.
Uchumi huangaliwa,
Mkazo ukatiliwa,
Pale nguvu zilokuwa,
Haraka za kuendelea.
422.
Mfano niliutoa,
Wa ujenzi Tanzania,
Watu tukawapatia,
Haraka nyumba kukaa.
423.
Itakuwepo mikoa,
Matofali yafyatua,
Na wengine kuuzia,
Kipato chao kikawa.
424.
Itakuwepo mikoa,
Samani inaandaa,
Milango kuiandaa,
Dirisha na kabati pia.
425.
Wengine wakanunua,
Mbao na kuzitumia,
Samani kujichongea,
Wenzao kuwauzia.
426.
Itakuwepo mikoa,
Vigae kujichomea,
Bilioni kufyatua,
Ujenzi ukaenea.
427.
Itakuwepo mikoa
Tailzi itachangia,
Uchumi tena kwa mia,
Ikawa wahesabiwa.
428.
Wataagizwa Songea,
Mafundi wa kujengea,
Ndanda na huko wajua,
Kwa wingi wakaajiriwa.
429.
Ikawa inachanua,
Hii yetu Tanzania,
Kwa umoja kujengewa,
Maskani tukakaa.
430.
Hali wanaajirwa,
kwa wingi waliokuwa,
Vijana wakitembea,
Pasi kazi kuijua.
431.
Uchumi ni kuamua,
Wapi tunaelekea,
Na siasa za ujamaa,
Kama bado zinafaa.
432.
Awali niliwambia,
Debe mie napigia,
Ubepari-ujamaa,
Siasa yetu ikawa.
433.
Na yake kubwa nadharia,
Ni uchumi huru kuwa,
Watu wakaruhusiwa,
Juu sana kujipandia.
434.
Juu sana kujipandia,
Pasiwe na kuzuiwa,
Ila kanuni kuzua,
Fukara kutoumia.
435.
Neti tutaiandaa,
Ya kiuchumi ilokuwa,
Kwa kodi kuzitumia,
Na maduhuli ya ubia.
436.
Navyo tuanvyojivunia,
Kwa dhahabu kuchimbua,
Na mali asili kuzaa,
Mfuko wa kusaidia.
437.
Elimu bure ikawa,
Usawa inayojua,
Hadi chuo kuingia,
Makato wakaanzia.
438.
Afya itaangaliwa,
Maskini kutodaiwa,
Wazazi kujifungua,
pasina kuwa udhia.
439.
Benki kuu kuandaa,
Kusaidia wazawa,
Ujasirmali kufaa,
Watu wakajinyanyua.
440.
Mitaji kupalilia,
Ya jamii ilokuwa,
Hapo tukaanzilia,
Kisha hatima kukua.
441.
Rasilimali radhia,
Watu wote kuwafaa,
Hao wanaoidokoa,
Budi kushughulikiwa.
442.
Yatakiwa Tanzania,
Mkakati nao kuwa,
Kukuza teknolojia,
Ili tusije chelewa.
443.
Rwanda tumeiachia,
Sasa yatutangulia,
Aibu ninajisikia,
Kila ninapojionea.
444.
Ilikuwa Tanzania,
Ya kwanza ingelikuwa,
Sera tuliiandaa,
Na kanuni kuanzia.
445.
Wanasiasa balaa,
Gurudumu wazuia,
Badala kuendelea,
Nyuma tunajirudia.
446.
Mamlaka yatakiwa,
Hili kulisimamia,
Huru itakayokuwa,
Si kama idara kuwa.
447.
Wajuzi wanatakiwa,
Mbele wanaoangalia,
Mambo wakayatambua,
Ielekeyako dunia.
448.
Vijitu tukitumia,
Vidudu tutabakia,
Nami sintoshangaa,
Zaidi tukilegea.
449.
Sera kubwa yatakiwa,
Vitu vingi kuvumbua,
Miaka iliyotimia,
Hamsini twaijua.
450.
Hamsini twaijua,
Toka uhuru kupewa,
Bado tuantegemea,
Vya nje kuvinunua?
451.
Aibu imetuishia,
Na haya twajiuzia,
Wataalamu wavia,
Kwa siasa kusambaa!
452.
Mipaka itanadiwa,
Utaalamu kupea,
Yake ukaangalia,
Na kilele kufikia.
453.
Siasa tukiachia,
Hazijengi, zabomoa,
Na taifa likavia,
Hadi tukalichukia.
454.
Trekta tungeanzia,
Katiba kulitambua,
La taifa latakiwa,
Humu humu likaundwa.
455.
Pampu zinatakiwa,
Viwanda vyetu kuzaa,
Fahari gani ikawa,
Paisna kujitegemea?
456.
Halafu ikafatia,
Nyumbu kuifufua,
Lori litakalokuwa,
Kama Yue Jin la China.
457.
Mikoa huru ikiwa,
Yatakiwa kuamua,
Uchumi kuwa ubia,
Wakazi ikanyanyua.
458.
Kuna mengi yanafaa,
Kwa pamoja kwandaliwa,
Kilimo, viwanda pia,
Uchumi kuustua.
459.
Aidha maji kujua,
Na wote yanatakiwa,
Ubia unapokuwa,
Shughuli huangaliwa.
460.
Umeme rahisi kuwa,
Ikizalisha mikoa,
Iweze kujitoshea,
Na mwingine kujiuzia.
461.
Viwanja vinatakiwa,
Kujengwa na kufufuliwa,
Hadhi ikajipandia,
Na wana kusaidia.
462.
Vyuo vikuu vyakua,
Kila mkoa vyatakiwa,
Ubia wakiingia,
Ugumu hawatojua.
463.
Na mikakati kutiwa,
Viongozi kuchagua,
Sio wa kuzawadiwa,
Ambao ni marejea.
464.
Masoko yakibuniwa,
Vitakiwavyo kutoa,
Hakuna kitachopungua,
Juu kupaa mikoa.
465.
Shule nzuri wakizua,
Nje watakujajisomea,
Ada wanayolipia,
Za kigeni kuingia.
466.
Hospitali kuzizua,
Wagonjwa wakatibiwa,
Nje waweza tokea,
Ikawa ni manufaa.
467.
Katiba inatakiwa,
Muongozo kuutoa,
Uchafu kuukata,
Tusiwe twavumilia.
468.
Miji yetu bora kuwa,
Na vijiji navyo pia,
Wazungu wakashangaa,
Wakadhania Ulaya.
469.
Ndani yetu limekaa,
Sio la kutegemea,
Siasa zinatakiwa,
Pembeni kuziambaa.
470.
Kubwa linalotakiwa,
Mitambo ya kurejelea,
Taka zilizoingia,
Zikageuzwa bidhaa.
471.
Seychelles naambiwa,
Mashine wajiundia,
Huko ningelitembea,
Badala kuranda Ulaya.
472.
Takataka tukijua,
Bidhaa zaweza kuwa,
Nyingine kurejelewa,
Vifaa tukatumia.
473.
Karatasi tukatoa,
Na plastiki nazo pia,
Na chupa kumiminiwa,
Kama mpya kurejea.
474.
Takataka ni mbolea,
Tena sumu isokuwa,
Sisi tunazichezea,
Na miji kuichafua.
475.
Mifereji tungejua,
Bayogesi ingetoa,
Chini kwa chini ikawa,
Mavuno twajivunia.
476.
Maji ya chumvi pia,
Baridi yaweza kuwa,
Nyumbani yakatumiwa,
Na shambani kumwagiwa.
477.
Katika ikichochea,
Haya yatagunduliwa,
Nchi ikajititimua,
Daraja bora ikawa.
478.
Kwa hayo tutatokea,
Mengine kuingilia,
Na watoto kuwaahcia,
Mengine wakagundua.
479.
Uhuru tukipanua,
Mengi tutajiundia,
Kuna wanaozaliwa,
Redio wajua tengeza!
480.
Ila wanadhulumiwa,
Na vifungo kutishiwa,
Hawa tungewaachia,
Mitambo watagundua.
481.
Kuna wanaopokea,
Cha wazungu nasikia,
Watoto kuwazuia,
Vya kwetu kuvivumbua.
482.
Katiba kuangalia,
Vipi twaweza kulea,
Wana wanaogundua,
Hadi tukavitumia.
483.
Wawe wasiouzuiwa,
Kisha ari kung'olewa,
Kama viza kutamiwa,
Kitu kisichoanguliwa ?
484.
Pasina wa kutamiwa,
Wanunuzi twabakia,
Katika hii hatua,
Vibovu watauuzia.
485.
Vyetu tukijiundia,
Vya ovyo havitakuwa,
Pia tutavielewa,
Na kurekebisha kwake.
486.
Gharama hatutaingia,
Nje kwanda agizia,
Maana ndani vyazaliwa,
Haja zetu kuzikidhi.
487.
Utamdauni wavia,
Baraza lasahauliwa,
Kichekesho kinakuwa,
Wazungu kuwategemea.
488.
Wazungu kuwategemea,
Utamaduni kulea,
Aibu imetupaa,
Na uso kuubinua?
489.
Utamaduni radhia,
Wazawa huangalia,
Na kinachotamaniwa,
Fungu pembeni kupewa.
490.
Ofisi zao kinyaa,
Kila idara na jaa,
Nani wa kuangalia,
Wote 'bize' wanakuwa?
491.
Na lugha tukianzia,
Ushauri nautoa,
katiba kuja amua,
Mamlaka yaundiwa.
492.
Mamlaka yaundiwa,
Huru itakayokuwa,
Kizibao kutovaa,
Wizara kutumikia.
493.
Mamlaka ya Kiswahili,
Itakuwa ni kamili,
Tena ni chombo halali,
Lugha kuiangalia.
494.
Vyanzo itachanganua,
Miradi kujianzishia,
Kipato kikaingia,
Yenyewe ikaamua.
495.
Ziengwe rasilimali,
Kutufaa bilkuli,
Sasa kwa ilivyo hali,
Ufisadi umejaa.
496.
Juu walojikweza,
Wataka kuzimaliza,
Wawa kama waigiza,
Ila wanatuchuuza.
497.
Mikataba waridhia,
Kama vile ya kijuha,
Au wananunuliwa,
Psina sisi kujua.
498.
Sasa kinachotakiwa,
Tamko leltu kutoa,
Rasilimali ni dia,
Twazimiliki raia.
499.
Pale kwetu tukivua,
Hiyo ni yetu ngekewa,
Mola katubarikia,
Japo hatukulijua.
500.
Iwepo asilimia,
Daima ya kuachiwa,
Kisha ndiyo kugaiwa,
Kitaifa Tanzania.
501.
Thamani kuichungua,
Iwe ni yetu tabia,
Na huo mtaji ukawa,
Kwa wazawa walokuwa.
502.
Waweza kujiuzia,
Au hisa kuridhia,
Umiliki wakajua,
Hali wanajinyanyua.
503.
Kijiji kikiamua,
Ubia kitawania,
Yao wakajifanyia,
Kisha wakajichomoa.
504.
Wakubwa wanayofanza,
Imani wanaikwaza,
Twaona wanajitunza,
Pekee wakajaliwa.
505.
Wao wakishapatiwa,
Sisi husahauliwa,
Mshirika wao kuwa,
Mwekezaji Tanzania.
506.
Tunaona wanapwaya,
Urahisi wanajitia,
Kidogo wanachopewa,
Sisi hatwezi kizaa ?
507.
Wanatakiwa kukua,
Njaa kuacha ugua,
Ili wapate tambua,
Tukijipanga twaweza.
508.
Wote tukijigawia,
Wala hakitapungua,
Na kinachowazuzua,
Kaburi lawaangia.
509.
Yatayokujakutokea,
Mazuri hayatakuwa,
Salama hapatakuwa,
Ila maisha kuvia.
510.
Vipaji vya tasnia,
Katiba inatakiwa,
Muongozo kuutoa,
Kwa haki vikalelewa.
511.
Sasa yanayotokea,
Mmoja mmoja kuwa,
Mwenyewe akiamua,
Nani kumsaidia.
512.
Mifumo kuandaliwa,
Vyote vikakaguliwa,
Na zikawepo sheria,
Hili kuliangalia.
513.
Watoto wa Tanzania,
Haki sawa watakiwa,
Pasiwe kupendelea,
Na wengine kuonewa.
514.
Vijana wa Tanzania,
Fursa sawa kupewa,
Sio kwa vitendo na nia,
Ila kwa kazi kufanziwa.
515.
Wazee wanatakiwa,
Baraza wakaundiwa,
Wala sio kutumiwa,
Kama vile kitambaa.
516.
Kama vile kitambaa,
Mikono kujifutia,
Ila wakatunukiwa,
Nchi kuizungumzia.
517.
Nchi kuizungmzia,
Pasina kuegemea,
Na kama ni kuamua,
Haki ikatangulia.
518.
Yao pia kwangalia,
Nafuu kujipatia,
Sasa wasahauiwa,
kila mtu anajua.
519.
Twaweza waangalia,
Mchabgo bora kutoa,
Nchi ikatengamaa,
Imara ipate kuwa.
520.
Wazee wamejaliwa,
Umri walioukaa,
Maisha wanayajua,
Na vituko kung'amua.
521.
Wasipokuwa na njaa,
Huingia ushujaa,
Udhia wakakataa,
Halali kupigania.
522.
Ndivyo inavyotakiwa,
Mchango bora kutoa,
Nchi ikaendelea,
Kwa aali nadharia.
523.
Kinamama watumiwa,
Na uchama kuwagawa,
Sasa fedha wagagawiwa,
Wengine kuwazomea.
524.
Vigelegele watia,
Ili wongo kufukia,
Kisha wakashangilia,
Ya haki yasiyokuwa.
525.
Baraza linatakiwa,
Zama lililoogopewa,
BAWATA kulifufua,
Umoja ikawania.
526.
Nchi hii yenye njaa,
Ujanja inatumia,
Wote wanaoishiwa,
Rahisi kununuliwa.
527.
Katiba inatakiwa,
Jambo hili kuzuia,
Kama ni kwendelea,
Juhudi zao kutia.
528.
Mambo ya
kunyanyuliwa,
Mengine yana udhia,
Mzungu twamnyania,
Yatakuja tuumbua.
529.
Katiba ingelifaa,
Majina kuyazuia,
Mwenyezi yanayomfaa,
Binadamu kutumia.
530.
Viongozi wakapewa,
Vichwani yakaingia,
Sumu kuwageukia,
Wakaiva kwa ubaya.
531.
Utukufu kuanzia,
Hilo kutoruhusiwa,
Qudusi aliyekuwa,
Mmoja mwingine hakuna.
532.
Mtakatifu hadaa,
Kiumbe hawezi kuwa,
Hili kutolitumia,
LIkakoleza balaa.
533.
Yatosha waheshimiwa,
Makengeza kutumia,
Hao ndio wahishimiwa,
Daima wanaoishiwa.
534.
Mwenyezi si wa kuishiwa,
Wala hawezi pungukiwa,
Sifa hiyo kajaliwa,
Binadamu alopewa.
535.
Mabunge tukijaliwa,
Aina mbili yakawa,
La wanaochaguliwa,
Na wanaoteuliwa.
536.
Maji kucha kutia,
Bunge la kuchaguliwa,
katiba ingekazia,
Vinginevyo kutokuwa.
537.
Watoto wanaumia,
Na sisi twaangalia,
Ukimwi kwa kuanzia,
Wazazi wawachukua.
538.
Hakuna lililokuwa,
Tayari tumelivumbua,
Kama chombo hicho
kuwa,
Hawa kuwaangalia.
539.
Inadorora jamii,
Kwa wakubwa kutotii,
Kiapo walichotanabahi,
Vyeoni wakiingia.
540.
Watu hawatumikii,
Kutumikiwa wadai,
Wakauzira uhai,
Na watu kuwachukia.
541.
Uongozi watakiwa,
Kiutu ulokomaa,
Usongoja kusifiwa,
Ila unaojitolea.
542.
Kinamama walofiwa,
Na waume nao pia,
Mayatima Tanzania,
Uyatima wakomaa.
543.
Nani wa kuwaangalia,
Ila wa kuwahurumia,
Katiba inatakiwa,
Hili likatatuliwa.
544.
Tunazo rasilimali,
Zinatosha kulhali,
Kushindwa uanzali,
Au utu watuishia.
545.
Hili pia laendana,
Nao mitaani wana,
Walikuwa wachache
jana,
Hivi leo ni mamia.
546.
Tutakuja pata laana,
Hili tusipolisana,
Yetu tukaharibiana,
Kwa hawa kuwaambaa.
547.
Watakuja
changanyikana,
Wakashidnwa elewana,
Wakaanza
kupambana,
Dhiki zikawanukia.
548.
Mifumo tumeishiwa,
Wala wengi hawajawa,
Ari tungelijaliwa,
Haya yasingetokea.
549.
Vijana twawaachia,
Paka tukawatishia,
Hofu zikiwaishia,
Tuna letu nawambia.
550.
Sasa kinachotakiwa,
Ni miundo kuzindua,
Na mifumo kufumua,
Upya tukajishonea.
551.
Hatuwezi tukalia,
Ajira zinapotea,
Na matatizo twajua,
Kedekede yamejaa.
556.
Mianya budi kutoa,
Wakubwa kupendelea,
Makwao kulikokuwa,
Jamhuri yote sawa.
557.
Fursa kutozuia,
Upinzani kuchanua,
Na wnakojishindia,
Nako kukaendelea.
558.
Matatizo Tanzania,
Fursa yaweza kuwa,
Vijana wakielewa,
Ajira kwao ikawa.
559.
Nyumba hatujajaliwa,
Na kiasi zapugnua,
Vijijini kunapwaya,
Si nyumba viota huwa.
560.
Miradi tukianzia,
Matofali kufyatua,
Benki kuu kwangalia,
Vipi itasaidia.
561.
Mikoa kuchaguliwa,
Watakaoyafyatua,
Na wengine wakawa,
Mengine wajifanyia.
562.
Vigae vinatakiwa,
Mkoa kazi kupewa,
Vijana ikatumia,
Wakajikimu kwa hili.
563.
Milango inatakiwa,
Na mbao waliokuwa,
Wataweza jiundia,
Au mbadala kuzua.
564.
Tailzi zinatakiwa,
Sakafuni zikatiwa,
Kama tukiazimia,
Vijana wataandaa.
565.
Dari watatengeneza,
Kwenye nyumba
kueneza,
Vijumba vikapendeza,
Na hadhi tukajipatia.
566.
Kilimo tukiamua,
Kitaajiri mamia,
Mtadi tukijitoa,
Kimasomaso ikawa.
567.
Msingi wakipatiwa,
Na chakula kugawia,
Wapo wataoridhia,
Kwenda kujitegemea.
568.
Na uvuvi nako pia,
Aidha na kujifugia,
Na viwanda kuvizua,
Vya msingi kuzalisha.
569.
Vijijini nawambia,
Kwingine kwanistua,
Milioni wakipewa,
Wanaweza kujitoa.
570.
Wanaweza kujitoa,
Uongozi wakipewa,
Haya unayoyajua,
Njia ukawaonyesha.
571.
Taasisi zimezuka,
Huko hazijawahi fika,
Elfu kumi zinataka,
Zikaweza kukomboa.
572.
Benki kuu ikitaka,
Mayai inayoweka,
Ikatamia hakika,
Nchi juu itapaa.
573.
Pesa kidogo ni dawa,
Matatizo kuondoa,
Masikini walokuwa,
Utajiri kunukia.
574.
Labda upo mwongozo,
Ulifanyalo mzozo,
Waogopa wenye nazo,
Umaskini ukiisha?
575.
Minong'ono yajaa,
Mtaji uliozuliwa,
Ni umasikini kulea,
Kutawala Tanzania.
576.
Makabila Tanzania,
Urithi tulojaliwa,
Uhaini kuyaua,
Kwa lolote lilokuwa.
577.
Umoja tumejaliwa,
Twajivuna Tanzania,
Kitakachouondoa,
Ufisadi si kabila.
578.
Matabaka yataua,
Si ukabila wa lugha,
Umoja tuliouzua,
Mbali wakajitupia.
579.
Rushwa itauondoa,
Si makabila Tanzania,
Kwa jinsi inavyoenea,
Na watu kuivumilia.
580.
Makabila kuenziwa,
Iwe ni yetu tabia,
Makumbusho yakapewa,
Kuhifadhi historia.
581.
Na kwayo teknolojia,
Lugha zikahifadhiwa,
Nani anayeyajua,
Mbele yatatusadiia?
582.
Kawaida ni sheria,
Kwa watu wasiojua,
Udini ukitumiwa,
Hili kuondoa baa!
583.
Wapo wanaojizuzua,
Kawaida kuiua,
Budi kushughulikiwa,
Ndiyo haki ilokuwa.
584.
Mapya tukizuia,
Kwa vitisho kutumia,
Raia watachukia,
Na kisasi kukitia.
585.
Watazidi kuroroma,
Na kuzizusha nakama.
Pakawepo uhasama,
Wa kijinga Tanzania.
586.
Mfano hili la kuchinja,
Wajua kina Masanja,
Dini moja walichinja,
Na wote tukaridhia.
587.
Ugumu halijakuwa,
Kuliko vita kuzua,
Serikali kuamua,
Pagani kuruhusiwa?
588.
Wagomvi wanaokua,
Vidogo huingilia,
Ukubwa wakautia,
Wapate kutambulika.
89.
Mabucha tukayatenga,
Yao yakatabandanga,
Na halali kuyakinga,
Yasije kuchafuliwa.
590.
Kuna wana Tanzania,
Wembe sasa walilia,
Kwa moja kuligundua,
Wadhani yote wajua.
591.
Kazi tukijipangia,
Na ufanisi zikawa,
Ufanifu nao pia,
Budi kuuangalia.
592.
Idadi ikizidia,
Kazi tunaichafua,
Kiasi inatakiwa,
Kutosha ni maridhia.
593.
Kisha wanaozipewa,
Kazi zao wakajua,
Sio kutunukiwa,
Madudu yatatujaa.
594.
Wajuzi waliokuwa,
Kazi zao kuachiwa,
Siasa zikiingilia,
Taifa hukorofisha.
595.
Ujira kuangalia,
Riziki ikatimia,
Kila inapopungua,
Uovu mpya huzua.
596.
Masoko yanatakiwa,
Kwa wakuu kuyajua,
Wasiishie tembea,
Pasina cha kujiuzia.
597.
Balozi zingetakiwa,
Rasimu kuiandaa,
Kila nchi tukajua,
Nini cha kujiuzia.
598.
Nini cha kujiuzia,
Na rahisi kununua,
Wasiishi na kukaa,
kama vile matajiri.
599.
Hujisahau balozi,
Nchi wakawa hawawazi,
Wakaishia usingizi,
Na tija usiokuwa.
600.
Kufunzwa wanatakiwa,
Ujasiramali tabia,
Kazini kuutumia,
Wakistaafu pia.
UTENZI WA KATIBA 601-799
601.
Bila hivyo hufulia,
Mengi yakawakimbia,
Na nchi kujikondea,
Minofu ikififia.
602.
Mawasiliano twajua,
Watu yanasaidia,
Na kilichobakia,
Unyonyaji kupungua.
607.
Fedha zikichukuliwa,
Na wachache walokuwa,
kawaida inakuwa,
Ni vibaya kutumiwa.
608.
Vocha bei kupungua,
Na muda kuongezewa,
kiasi kitabakia,
Mengine kujifanyia.
609.
Dijito teknolojia,
Jinsi ninavyoelewa,
Urahisi yatakiwa,
Maisha kutufanyia.
610.
Ujanja ukipungua,
Gharama haitakuwa,
Mbadala kujaliwa,
Kawaida kurejea.
611.
Ila tukiwaachia,
Wajanja waliokuwa,
Pasina kuwa sheria,
Hili kuliangalia.
612.
Kwa miaka kama mia,
Mlaji kumrarua,
Hii ndiyo dunia,
Mabepari twawajua.
613.
Kompyuta Tanzania,
Budi kujitengezea,
Zetu zilizokuwa,
Kiswahili zatumia.
614.
Ni lugha iliyokuwa,
Kila mtu atumia,
Mwanzo wameanzia,
Wenye simu twasifia.
615.
Sasa ni kufatia,
Kompyuta kutumia,
Na mtandao ukawa,
Kiswahili kidedea!
616.
Vizuri tukijitoa,
Vyuo tutavifungua,
Kwa tovuti kutumia,
Afrika kuenea.
617.
Na ajira zikajaa,
Afika kufunzia,
Kiswahili kikakua,
Na uchumi kuinua.
618.
Nacho tusichojaliwa,
Viongozi wakujua,
Njia wanaotambua,
Wapi pa kuelekea.
619.
Vijiji kubwa hazina,
Kuvitunza vikafana,
Tena pasina hiyana,
Kwani tumevionea.
620.
Huduma nyingi zavia,
Kila mtu anajua,
Muongo unatakiwa,
Haya tuawapatia.
621.
Maji kutiririka,
Vijijini tunataka,
Waache kuhangaika,
Kinamama kuadhirika.
622.
Umeme kutochelewa,
Nyuma ukayafatia,
Gizani hatukuumbiwa,
Ni nani asiyejua.
623.
Nyumba nimeongelea,
Zastahili familia,
Kwa mbinu kujengewa,
Na ajira zikatoa.
624.
Hayo yakishakuwa,
Ndege yetu itapaa,
Mengine kuangalia,
Hali bora kufikia.
625.
Takwimu za Tanzania,
Watu shaka watilia,
Katiba ingetwakiwa,
Na hili kuliondoa.
626.
Ninachofikiria,
Mamlaka kuundiwa,
Na mtu isoingiliwa,
Kazi ikajifanzia.
627.
Kwa hivyo kuaminiwa,
Uhuru ikishajaliwa,
Jukumu ikalipewa,
Ukweli kupigania.
628.
Uongo kukaataa,
Na waongo kuumbua,
Mkuu hadhi akawa,
Katiba kumwangalia.
629.
Ya vyama yasiyofaa,
Hayo tutayaambaa,
Na ikulu ya kuzua,
Ukweli tukaujua.
630.
Ya tume yenye hadaa,
Yote tukayafichua,
Sensa bora kujaliwa,
Muongo kat ukiwa.
631.
Dawa tungejitambua,
Mbali tungeishakua,
Uizi uliingia,
Hakuna wa kuaminiwa.
632.
Katiba inatakiwa,
Wa jadi kuangalia,
Na msaada kupewa,
Vyao wakajiundia.
633.
Za asili tungetoa,
Na za kisasa kuzua,
Kama Wachina tukawa,
Uchumi tukajaliwa.
634.
Hakika hapa twapwaya,
Ila cha babu kikiwa,
Sasa kinachosahauliwa,
Na kingine kungojewa.
635.
Mavazi hatujaamua,
Na miaka yaishia,
Ni sanaa imekuwa,
Ndee-nani ayajua!
636.
Inacheka historia,
Kigugumizi kikiwa,
Wapi tulipopotea,
Ila usanii kuvaa?
637.
Thamani inatakiwa,
Ya mzawa Tanzania,
Vipi Mwadui akawa,
Sawa na kusikokuwa.
638.
Na thamani ni uchumi,
Ardhini uliokuwa,
Huo ukichanganuliwa,
Mwananchi akapewa.
639.
Ya Wazungu na Asia,
Mabwana wakaja kuwa,
Hapo wasingefikia,
Na thamani tungekuwa.
640.
Saluti tungepigiwa,
Kama kwa wenye kujua,
Waarabu maridhia,
Sana wanaheshimiwa.
641.
Qatar ukiingia,
Na Dubai nako pia,
Hili utaligundua,
Wivu ukakuingia.
642.
Imeshazuka tabia,
Wakubwa kujifanzia,
Bila sisi kuyajua,
Na kisha kudharauliwa.
643.
Na kisha kudahauliwa,
Na matusi kutupiwa,
Hili ninawaambia,
Kubaya twaelekea.
644.
Mtu hauwezi kuwa,
Pasina na watu kuwa,
Ukitaka kulijua,
Porini ukitupiwa.
645.
Wakubwa mngerejea,
Nafsi kuziangalia,
Ukubwa sio kupaa,
Au malaika kuwa.
646.
Ni watu wa kujijua,
Ndio nchi hujaliwa,
Ila wasiojitambua,
Kwao nchi huangamia.
647.
Mtakatifu hujawa,
Hadi unapojifia,
Ulimi ukiamua,
Unaweza kuchafua.
648.
Unaweza kuchafua,
Na motoni kwenda kaa,
Mazuri uliyodhania,
Yote yakawa kinyaa.
649.
Ni chafu historia,
Ya nchi hii Tanzania,
Ushiriki ni tanzia,
Kuzikwa ulishajifia.
650.
Mchezo wakichezewa,
Enzi zilotangulia,
Pahala wakaishia,
Vijiji vikawa baa!
651.
Kinyume kiangalia,
Yahudi wametimia,
Vyao wamevinyanyua,
Kitega uchumi kuwa.
652.
Sisi tuliochezea,
Shilingi tukaachia,
Chooni ikaingia,
Twawa ni wa kufulia.
653.
Tulichokikosea,
Raia tulihadaa,
Kwa king'enge kwishia:
'Manipulation' hatua.
654.
Tiba hatukuijua,
Therapy kufafanuliwa,
Tukaganga yetu nia,
Na nyufa kuzitumia.
655.
Taarifa nayo pia,
Hiyo hatukuifikia,
Kwani tulipoishia,
Hatujui ni 'Informing'.
656.
Leo ukitembelea,
Vijiji vya Tanzania,
Ufahamu wafulia,
Ila tu yao kujua.
657.
Kwao ni giza dunia,
Mawasiiano sanaa,
Kwa simu isipokuwa,
Na mnara palokuwa.
658.
Yao wakaongelea,
Na umbeya kuupokea,
Ila habari kujua,
Bado wanatahiniwa.
659.
Ushauri umevia,
Nani watakusikia,
Imeshazuka tabia,
Kila kitu wanajua.
660.
Wazo ukiwaachia,
Haraka watakuibia,
Mkia wakauchukua,
kishwa wakakuachia.
661.
Nusunusu huyazua,
Ndio kufa kuwa kawa,
Nam sintosikitikia,
Pasi katiba kuwa dawa.
662.
Kwingine tukachagua,
Kwenda kuchangamkia,
Kura tukajiombea,
Ndiko kulikoendelea.
663.
Na mtu wasiyekuwa,
Au uoga kwingia,
Nyuma tukishabakia,
Huko si kuendelea.
664.
Hatua zinazotakiwa,
Ni ubia kuingia,
Pamoja wakayazua,
Nchi yatayonyanyua.
665.
Hapo wakishafikia,
Mamlaka kukaimiwa,
Huru ikiwa mikoa,
kasi yetu ya kupaa.
666.
Ushindani ukiingia,
Wa kweli uliokuwa,
Wavivu watajijua,
Wenyewe kujiondoa.
667.
Wabebwa watang'aamua,
Ngazi wakaziachia,
Barubaru wakatwaa,
Kilele kuelekea.
668.
Imekua Tanzania,
Nje budi kuingia,
Biashara kuzizua,
Na kampuni kwanzisha.
669.
Bakhresa kawa ni taa,
Njia anazipasua,
Wivu kutokumuonea,
Ila tuwe twamsaidia.
670.
CRFB wapaa,
Burundi weshaingia,
Afrika kuenea,
Pengine waazimia.
671.
Katiba ikichochea,
Kupanuka tasnia,
Makampuni Tanzania,
Kimataifa yakawa.
672.
Hilo jema lingekuwa,
Na chati kutunyanyua,
Watoto kuajirriwa,
Nchi za nje kukaa.
673.
Lugha watajisomea,
Zitawalazo dunia,
Kizulu wakakijua,
Sambamba nacho Kichina.
674.
Kihausa kukijua,
Na Kiarabu nacho pia,
Kazi wakajifanzia,
Zing'arishazo Tanzania.
675.
Hatua itafikiwa,
Umma upate chipua,
Mamlaka kuyagawa,
Washike Watanzania.
676.
Hapo watakaobakia,
Si rushwa waliotoa,
Ila wanaojijua,
Na wajibu kutimia.
677.
Umaskini uchafu,
Unayo mbaya harufu,
Hili kujitaarifu,
Wote tukalikataa.
678.
Kuna wanaotumia,
Kuyapata manufaa,
Hao ni kuwashushua,
Akili zikarejea.
679.
Ziengwe rasilimali,
Kutufaa bilkuli,
Sasa kwa ilivyo hali,
Ufisadi umejaa.
680.
Juu walojikweza,
Wataka kuzimaliza,
Wawa kama waigiza,
Ila wanatuchuuza.
681.
Mikataba waridhia,
Kama vile ya kijuha,
Au wananunuliwa,
Psina sisi kujua.
682.
Sasa kinachotakiwa,
Tamko leltu kutoa,
Rasilimali ni dia,
Tunazimiliki raia.
683.
Pale kwetu tukivua,
Hiyo ni yetu ngekewa,
Mola katubarikia,
Japo hatukulijua.
684.
Iwepo asilimia,
Daima ya kuachiwa,
Kisha ndiyo kugaiwa,
Kitaifa Tanzania.
685.
Thamani kuichungua,
Iwe ni yetu tabia,
Na huo mtaji ukawa,
Kwa wazawa walokuwa.
686.
Waweza kujiuzia,
Au hisa kuridhia,
Umiliki wakajua,
Hali wanajinyanyua.
687.
Kijiji kikiamua,
Ubia kitawania,
Yao wakajifanyia,
Kisha wakajichomoa.
688.
kubwa wanayofanza,
Imani wanaikwaza,
Twaona wanajikweza,
Pekee wakajaliwa.
689.
Wao wakishapatiwa,
Sisti husahauliwa,
Mshirika wao kuwa,
Mwekezaji Tanzania.
690.
Tunaona wanapwaya,
Urahisi wanajitia,
Kidogo wanachochukua,
Mbona twaweza chimbua?
691.
Wanatakiwa kukua,
Njaa kuacha ugua,
Ili wapate tambua,
Ufakiri si laana.
692.
Wote tukijigawia,
Wala hautapungua,
Na kichowazuzua,
Kaburi wakimbilia.
693.
Yatayokujakutokea,
Mazuri hayatakuwa,
Salama hapatakuwa,
Ila maisha kuvia.
694.
Vipaji vya tasnia,
Katiba inatakiwa,
Muongozo kuutoa,
Kwa haki vikalelewa.
695.
Sasa yanayotokea,
Mmoja mmoja kuwa,
Mwenyewe akiamua,
Nani kumsaidia.
696.
Mifumo kuandaliwa,
Wote wakashughulikiwa,
Na zikawepo sheria,
Hili kuliangalia.
697.
Watoto wa Tanzania,
Haki sawa watakiwa,
Pasiwe kupendelea,
Na wengine kuonewa.
698.
Vijana wa Tanzania,
Fursa sawa kupewa,
Sio kwa vitendo na nia,
Ila kwa kazi kufanziwa.
699.
Wazee wanatakiwa,
Baraza wakaundiwa,
Wala sio kutumiwa,
Kama vile kitambaa.
700.
Kama vile kitambaa,
Mikono kujifutia,
Ila wakatunukiwa,
Nchi kuizungumzia.
701.
Nchi kuizungmzia,
Pasina kuegemea,
Na kama ni kuamua,
Haki ikawatangulia.
702.
Yao pia kwangalia,
Nafuu kujipatia,
Leo wasahauiwa,
kila mtu anajua.
703.
Twaweza kuwafufua,
Mchango bora kutoa,
Nchi ikatengamaa,
Na imara kwenda kuwa.
704.
Wazee wamejaliwa,
Umri walioukaa,
Maisha wanayajua,
Na vituko kung'amua.
705.
Wasipokuwa na njaa,
Huingia ushujaa,
Udhia wakakataa,
Halali kupigania.
706.
Ndivyo inavyotakiwa,
Mchango bora kutoa,
Nchi ikaendelea,
Kwa aali nadharia.
707.
Kinamama Tanzania,,
Makubwa wangetufanyia,
Wenyewe wangejijua,
Wala sio kutumiwa.
708.
Taasisi yatakiwa,
Kufunzwa sosholojia,
Pia na saikolojia,
Waweze kujikomboa.
709.
Kisha wakaongezewa,
Uongozi kuujua,
Na fitina wakatoa,
Wenyewe kujipendelea.
710.
Wajanja wakizaliwa,
Watu hutaka nunua,
Bei wakajipangia,
Ili yao kutimia.
711.
Husahau yakujua,
Hadi wakaulizia,
Hususan inapokuwa,
Magogo wanawekewa.
712.
Upande wanaujua,
Sana uliolegea,
Hukohuko huingia,
Vibeti kuvibetua.
713.
Sasa nchi yatakiwa,
Wananchi kuamua,
Si kugeuzwa majuha,
Mambo wakalazimishwa.
714.
Vikundi kuzinduliwa,
Jamii ikavitumia,
Yao kuyapigania,
Pasina kuingiliwa.
715.
Mgao ukitokea,
Watu wanaonunua,
Na wanaokataa,
Wao kutonunuliwa.
716.
Kuuzwa wanaokataa,
Sauti pia kusikiwa,
Sio tu mkawafaa,
Wanaotaka nunua.
717.
Ustawi wa jamii,
Kama hai silijui,
Naona haina uhai,
Kwa yanayoendelea.
718.
Juhudi zinatakiwa,
Idara kuiangalia,
Hapo ilipotiwa,
Naona inazidiwa.
719.
Idara ingelikuwa,
Mamlaka Tanzania,
Kaziye kuangalia,
Wanyonge waliokuwa.
720.
Kinamama walofiwa,
Na waume nao pia,
Mayatima Tanzania,
Uyatima wakomaa.
721.
Nani wa kuwaangalia,
Ila wa kuwahurumia,
Katika inatakiwa,
Hili likatatuliwa.
722.
Tunazo rasilimali,
Zinaosha kulhali,
Kushindwa uanzali,
Au utu watuishia.
723.
Hili pia laendana,
Na wa mitaani wana,
Walikuwa wachache jana,
Hivi leo ni mamia.
724.
Tutakuja pata laana,
Hili tusipolisana,
Yetu tukaharibiana,
Kwa hawa kuwaambaa.
725.
Watakuja changanyikana,
Wakashidnwa elewana,
Hepu wakaanza pambana,
Dhiki zikawanukia.
726.
Mifumo tumeishiwa,
Wala wengi hawajawa,
Ari tungelijaliwa,
Haya yasingetokea.
727.
Vijana twawaachia,
Paka tukawatishia,
Hofu zikiwaishia,
Tuna letu nawambia.
728.
Sasa kinachotakiwa,
Ni miundo kuzindua,
Na mifumo kufumua,
Upya tukajishonea.
729.
Hatuwezi tukalia,
Ajira zinapotea,
Na matatizo twajua,
Kedekese yamejaa.
730.
Matatizo Tanzania,
Fursa yaweza kuwa,
Vijana wakielewa,
Ajira kwao ikawa.
731.
Nyumba hatujajaliwa,
Na kiasi zapugnua,
Vijijini ni balaa,
Si nyumba viota huwa.
732.
Viwanda tukianzia,
Mbali mbali vyatakiwa,
Si wote moja kuzaa,,
Uzalshaji kugawa.
732.
Mikoa kuchaguliwa,
Viwanda -mbao kuwa,
Ubora wakishakuwa,
Dunia kuwanunua.
733.
Vya vyuma vinatakiwa,
Mali ghafi kuzitoa,
Wengine wakanunua,
Yao kujitengezea.
734.
Na vyakula navyo pia,
Viwanda vyake vyafaa,
Pahala tukachagua,
Rahisi panapokuwa.
735.
Aidha vinywaji pia,
Mikoa tungechagua,
Hyo ikatuzalishia,
Tusambaze TanZania.
736.
Saruji nayo mbolea,
Hivyo hivyo kuvigawa,
Pamoja vinapokaa,
Gharama zinapungua.
737.
Kilimo tukiamua,
Kitaajiri mamia,
Mtadi tukijitoa,
Kimasomaso ikawa.
738.
Msingi wakipatiwa,
Na chakula kugawia,
Wapo wataoridhia,
Kwenda kujitegemea.
Na uvuvi nako pia,
idha na kujifugia,
Na viwanda kuvizua,
Vya msingi kuzalisha.
739.
Vijijini nawambia,
Kwingine kwanistua,
Milioni wakipewa,
Wanaweza kujitoa.
740.
Wanaweza kujitoa,
Uongozi wakipewa,
Haya unayoyajua,
Njia ukawaonyesha.
741.
Taasisi zimezuka,
Huko hazijawahi fika,
Elfu kumi zinataka,
Zikaweza kukomboa.
742.
Benki kuu ikitaka,
Mayai inayoweka,
Ikatamia hakika,
Nchi juu itapaa.
Pesa kidogo ni dawa,
Mtizo kuondoa,
Masikini walokuwa,
Utajiri kunukia.
743.
Labda upo mwongozo,
Ulifanyalo mzozo,
Waogopa wenye nazo,
Umaskini ukiisha?
744.
Minong'ono yajaa,
Mtaji uliozuliwa,
Ni umasikini kulea,
Kutawala Tanzania.
745.
Makabila Tanzania,
Urithi tulojaliwa,
Uhaini kuyaua,
Kwa lolote lilokuwa.
746.
Umoja tumejaliwa,
Twajivuna Tanzania,
Na kitakachoundoa,
Ufisadi si kabila.
747.
Matabaka yataua,
Si ukabila wa lugha,
Umoja tuliouzua,
Mbali wakajitupia.
748.
Rushwa itauondoa,
Si makabila Tanzania,
Kwa jinsi inavyoenea,
Na watu kuivumilia.
749.
Makabila kuenziwa,
Iwe ni yetu tabia,
Makumbusho yakapewa,
Kuhifadhi historia.
750.
Na kwayo teknolojia,
Lugha zikahifadhiwa,
Nani anayeyajua,
Mbele vitatusadiia?
751.
Kawaida ni sheria,
Kwa watu wasiojua,
Udini ukitumiwa,
Hili kuondoa baa!
752.
Wapo wanaojizuzua,
Kawaida kuiua,
Budi kushughulikiwa,
Ndiyo haki ilokuwa.
753.
Mapya tukillia,
Na vitisho kutmia,
Wajinga waliokuwa,
Wataona wasikiwa.
754.
Watazidi kuroroma,
Na kuzizusha nakama.
Pakawepo uhasama,
Wa kijinga Tanzania.
755.
Mfano hili la kuchinja,
Wajua kina Masanja,
Dini moja walichinja,
Na wote tukaridhia.
756.
Ugumu halijakuwa,
Kuliko vita kuzua,
Serikali kuamua,
Kafiri kuruhusiwa.
757.
Ila tangazo kutoa,
Hakuchinjwa kauiwa,
Mnyama aliyekuwa,
Si halali kununua.
758.
Mabucha tukayatenga,
Yao yakatabandanga,
Na halali kuyakinga,
Yasije kuchafuliwa.
759.
Kuna wana Tanzania,
Wembe sasa walilia,
Kwa moja kuligundua,
Wadhani yote wajua.
760.
Kazi tukijipangia,
Na ufanisi zikawa,
Ufanifu nao pia,
Budi kuuangalia.
761.
Idadi ikizidia,
Kazi tunaichafua,
Kiasi inatakiwa,
Kutosha ni maridhia.
762.
Kisha wanaozipewa,
Kazi zao wakajua,
Sio kutunukiwa,
Madudu yatatujaa.
763.
Wajuzi waliokuwa,
Kazi zao kuachiwa,
Siasa zikiingilia,
Taifa hukorofisha.
764
Ujira kuangalia,
Riziki ikatimia,
Kila inapopungua,
Uovu mpya huzua.
765.
Masoko yanatakiwa,
Kwa wakuu kuyajua,
Wasiishie tembea,
Pasina cha kujiuzia.
766.
Balozi zingetakiwa,
Rasimu kuiandaa,
Kila nchi tukajua,
Nini cha kujiuzia.
767.
Nini cha kujiuzia,
Na rahisi kununua,
Wasiishi na kukaa,
kama vile matajiri.
768.
Hujisahau balozi,
Nchi wakawa hawawazi,
Wakaishia usingizi,
Na tija usiokuwa.
769.
Kufunzwa wanatakiwa,
Ujasiramali tabia,
Kazini kuutumia,
Wakistaafu pia.
770.
Bila hivyo hufulia,
Mengi yakawakimbia,
Na nchi kujikondea,
Minofu ikififia.
771.
Mawasiliano twajua,
Watu yanasaidia,
Na kilichobakia,
Unyonyaji kupungua.
772.
Hela zikichukuliwa,
Na wachache walokuwa,
kawaida inakuwa,
Ni vibaya kutumiwa.
773.
Vocha bei kupungua,
Na muda kuongezewa,
kiasi kitabakia,
Mengine kujifanyia.
774.
Dijito teknolojia,
Jinsi ninavyoelewa,
Urahisi yatakiwa,
Maisha kutufanyia.
775.
Ujanja ukipungua,
Gharama haitakuwa,
Mbadala kujaliwa,
Kawaida kurejea.
776.
Ila tukiwaachia,
Wajanja waliokuwa,
Pasina kuwa sheria,
Hili kuliangalia.
777.
Kwa miaka kama mia,
Mlaji kumrarua,
Hii ndiyo dunia,
Mabepari twawajua.
778.
Kompyuta Tanzania,
Budi kujitengezea,
Zetu zilizokuwa,
Kiswahili zatumia.
779.
Ni lugha iliyokuwa,
Kila mtu atumia,
Mwanzo wameanzia,
Wenye simu twasifia.
780.
Sasa ni kufatia,
Kompyuta kutumia,
Na mtandao ukawa,
Kiswahili kidedea!
781.
Vizuri tukijitoa,
Vyuo tutavifungua,
Kwa tovuti kutumia,
Afrika kuenea.
782.
Na ajira zikajaa,
Afika kufunzia,
Kiswahili kikakua,
Na uchumi kuinua.
783.
Nacho tusichojaliwa,
Viongozi wakujua,
Njia wanaotambua,
Wapi pa kuelekea.
784.
Vijiji kubwa hazina,
Kuvitunza vikafana,
Tena pasina hiyana,
Kwani tumevionea.
785.
Huduma nyingi zavia,
Kila mtu anajua,
Muongo unatakiwa,
Haya tuawapatia.
786.
Maji kutiririka,
Vijijini tunataka,
Waache kuhangaika,
Kinamama kuadhirika.
787.
Umeme kutochelewa,
Nyuma ukayafatia,
Gizani hatukuumbiwa,
Ni nani asiyejua.
788.
Nyumba nimeongelea,
Zastahili familia,
Kwa mbinu kujengewa,
Na ajira zikatoa.
790.
Hayo yakishakuwa,
Ndege yetu itapaa,
Mengine kuangalia,
Hali bora kufikia.
791.
Takwimu za Tanzania,
Watu shaka watilia,
Katiba ingetwakiwa,
Na hili kuliondoa.
792.
Ninachofikiria,
Mamlaka kuundiwa,
Na mtu isoingiliwa,
Kazi ikajifanzia.
793.
Kwa hivyo kuaminiwa,
Uhuru ikishajaliwa,
Jukumu ikalipewa,
Ukweli kupigania.
794.
Uongo kukaataa,
Na waongo kuumbua,
Mkuu hadhi akawa,
Katiba kumwangalia.
795.
Ya vyama yasiyofaa,
Hayo tutayaambaa,
Na ikulu ya kuzua,
Ukweli tukaujua.
796.
Ya tume yenye hadaa,
Yote tukayafichua,
Sensa bora kujaliwa,
Muongo kat ukiwa.
797.
Dawa tungejitambua,
Mbali tungeishakua,
Uizi uliingia,
Hakuna wa kuaminiwa.
798.
Katiba inatakiwa,
Wa jadi kuangalia,
Na msaada kupewa,
Vyao wakajiundia.
799.
Za asili tungetoa,
Na za kisasa kuzua,
Kama Wachina tukawa,
Uchumi tukajaliwa.
UTENZI WA KATIBA 601-799
601.
Bila hivyo hufulia,
Mengi yakawakimbia,
Na nchi kujikondea,
Minofu ikififia.
602.
Mawasiliano twajua,
Watu yanasaidia,
Na kilichobakia,
Unyonyaji kupungua.
607.
Fedha zikichukuliwa,
Na wachache walokuwa,
kawaida inakuwa,
Ni vibaya kutumiwa.
608.
Vocha bei kupungua,
Na muda kuongezewa,
kiasi kitabakia,
Mengine kujifanyia.
609.
Dijito teknolojia,
Jinsi ninavyoelewa,
Urahisi yatakiwa,
Maisha kutufanyia.
610.
Ujanja ukipungua,
Gharama haitakuwa,
Mbadala kujaliwa,
Kawaida kurejea.
611.
Ila tukiwaachia,
Wajanja waliokuwa,
Pasina kuwa sheria,
Hili kuliangalia.
612.
Kwa miaka kama mia,
Mlaji kumrarua,
Hii ndiyo dunia,
Mabepari twawajua.
613.
Kompyuta Tanzania,
Budi kujitengezea,
Zetu zilizokuwa,
Kiswahili zatumia.
614.
Ni lugha iliyokuwa,
Kila mtu atumia,
Mwanzo wameanzia,
Wenye simu twasifia.
615.
Sasa ni kufatia,
Kompyuta kutumia,
Na mtandao ukawa,
Kiswahili kidedea!
616.
Vizuri tukijitoa,
Vyuo tutavifungua,
Kwa tovuti kutumia,
Afrika kuenea.
617.
Na ajira zikajaa,
Afika kufunzia,
Kiswahili kikakua,
Na uchumi kuinua.
618.
Nacho tusichojaliwa,
Viongozi wakujua,
Njia wanaotambua,
Wapi pa kuelekea.
619.
Vijiji kubwa hazina,
Kuvitunza vikafana,
Tena pasina hiyana,
Kwani tumevionea.
620.
Huduma nyingi zavia,
Kila mtu anajua,
Muongo unatakiwa,
Haya tuawapatia.
621.
Maji kutiririka,
Vijijini tunataka,
Waache kuhangaika,
Kinamama kuadhirika.
622.
Umeme kutochelewa,
Nyuma ukayafatia,
Gizani hatukuumbiwa,
Ni nani asiyejua.
623.
Nyumba nimeongelea,
Zastahili familia,
Kwa mbinu kujengewa,
Na ajira zikatoa.
624.
Hayo yakishakuwa,
Ndege yetu itapaa,
Mengine kuangalia,
Hali bora kufikia.
625.
Takwimu za Tanzania,
Watu shaka watilia,
Katiba ingetwakiwa,
Na hili kuliondoa.
626.
Ninachofikiria,
Mamlaka kuundiwa,
Na mtu isoingiliwa,
Kazi ikajifanzia.
627.
Kwa hivyo kuaminiwa,
Uhuru ikishajaliwa,
Jukumu ikalipewa,
Ukweli kupigania.
628.
Uongo kukaataa,
Na waongo kuumbua,
Mkuu hadhi akawa,
Katiba kumwangalia.
629.
Ya vyama yasiyofaa,
Hayo tutayaambaa,
Na ikulu ya kuzua,
Ukweli tukaujua.
630.
Ya tume yenye hadaa,
Yote tukayafichua,
Sensa bora kujaliwa,
Muongo kat ukiwa.
631.
Dawa tungejitambua,
Mbali tungeishakua,
Uizi uliingia,
Hakuna wa kuaminiwa.
632.
Katiba inatakiwa,
Wa jadi kuangalia,
Na msaada kupewa,
Vyao wakajiundia.
633.
Za asili tungetoa,
Na za kisasa kuzua,
Kama Wachina tukawa,
Uchumi tukajaliwa.
634.
Hakika hapa twapwaya,
Ila cha babu kikiwa,
Sasa kinachosahauliwa,
Na kingine kungojewa.
635.
Mavazi hatujaamua,
Na miaka yaishia,
Ni sanaa imekuwa,
Ndee-nani ayajua!
636.
Inacheka historia,
Kigugumizi kikiwa,
Wapi tulipopotea,
Ila usanii kuvaa?
637.
Thamani inatakiwa,
Ya mzawa Tanzania,
Vipi Mwadui akawa,
Sawa na kusikokuwa.
638.
Na thamani ni uchumi,
Ardhini uliokuwa,
Huo ukichanganuliwa,
Mwananchi akapewa.
639.
Ya Wazungu na Asia,
Mabwana wakaja kuwa,
Hapo wasingefikia,
Na thamani tungekuwa.
640.
Saluti tungepigiwa,
Kama kwa wenye kujua,
Waarabu maridhia,
Sana wanaheshimiwa.
641.
Qatar ukiingia,
Na Dubai nako pia,
Hili utaligundua,
Wivu ukakuingia.
642.
Imeshazuka tabia,
Wakubwa kujifanzia,
Bila sisi kuyajua,
Na kisha kudharauliwa.
643.
Na kisha kudahauliwa,
Na matusi kutupiwa,
Hili ninawaambia,
Kubaya twaelekea.
644.
Mtu hauwezi kuwa,
Pasina na watu kuwa,
Ukitaka kulijua,
Porini ukitupiwa.
645.
Wakubwa mngerejea,
Nafsi kuziangalia,
Ukubwa sio kupaa,
Au malaika kuwa.
646.
Ni watu wa kujijua,
Ndio nchi hujaliwa,
Ila wasiojitambua,
Kwao nchi huangamia.
647.
Mtakatifu hujawa,
Hadi unapojifia,
Ulimi ukiamua,
Unaweza kuchafua.
648.
Unaweza kuchafua,
Na motoni kwenda kaa,
Mazuri uliyodhania,
Yote yakawa kinyaa.
649.
Ni chafu historia,
Ya nchi hii Tanzania,
Ushiriki ni tanzia,
Kuzikwa ulishajifia.
650.
Mchezo wakichezewa,
Enzi zilotangulia,
Pahala wakaishia,
Vijiji vikawa baa!
651.
Kinyume kiangalia,
Yahudi wametimia,
Vyao wamevinyanyua,
Kitega uchumi kuwa.
652.
Sisi tuliochezea,
Shilingi tukaachia,
Chooni ikaingia,
Twawa ni wa kufulia.
653.
Tulichokikosea,
Raia tulihadaa,
Kwa king'enge kwishia:
'Manipulation' hatua.
654.
Tiba hatukuijua,
Therapy kufafanuliwa,
Tukaganga yetu nia,
Na nyufa kuzitumia.
655.
Taarifa nayo pia,
Hiyo hatukuifikia,
Kwani tulipoishia,
Hatujui ni 'Informing'.
656.
Leo ukitembelea,
Vijiji vya Tanzania,
Ufahamu wafulia,
Ila tu yao kujua.
657.
Kwao ni giza dunia,
Mawasiiano sanaa,
Kwa simu isipokuwa,
Na mnara palokuwa.
658.
Yao wakaongelea,
Na umbeya kuupokea,
Ila habari kujua,
Bado wanatahiniwa.
659.
Ushauri umevia,
Nani watakusikia,
Imeshazuka tabia,
Kila kitu wanajua.
660.
Wazo ukiwaachia,
Haraka watakuibia,
Mkia wakauchukua,
kishwa wakakuachia.
661.
Nusunusu huyazua,
Ndio kufa kuwa kawa,
Nam sintosikitikia,
Pasi katiba kuwa dawa.
662.
Kwingine tukachagua,
Kwenda kuchangamkia,
Kura tukajiombea,
Ndiko kulikoendelea.
663.
Na mtu wasiyekuwa,
Au uoga kwingia,
Nyuma tukishabakia,
Huko si kuendelea.
664.
Hatua zinazotakiwa,
Ni ubia kuingia,
Pamoja wakayazua,
Nchi yatayonyanyua.
665.
Hapo wakishafikia,
Mamlaka kukaimiwa,
Huru ikiwa mikoa,
kasi yetu ya kupaa.
666.
Ushindani ukiingia,
Wa kweli uliokuwa,
Wavivu watajijua,
Wenyewe kujiondoa.
667.
Wabebwa watang'aamua,
Ngazi wakaziachia,
Barubaru wakatwaa,
Kilele kuelekea.
668.
Imekua Tanzania,
Nje budi kuingia,
Biashara kuzizua,
Na kampuni kwanzisha.
669.
Bakhresa kawa ni taa,
Njia anazipasua,
Wivu kutokumuonea,
Ila tuwe twamsaidia.
670.
CRFB wapaa,
Burundi weshaingia,
Afrika kuenea,
Pengine waazimia.
671.
Katiba ikichochea,
Kupanuka tasnia,
Makampuni Tanzania,
Kimataifa yakawa.
672.
Hilo jema lingekuwa,
Na chati kutunyanyua,
Watoto kuajirriwa,
Nchi za nje kukaa.
673.
Lugha watajisomea,
Zitawalazo dunia,
Kizulu wakakijua,
Sambamba nacho Kichina.
674.
Kihausa kukijua,
Na Kiarabu nacho pia,
Kazi wakajifanzia,
Zing'arishazo Tanzania.
675.
Hatua itafikiwa,
Umma upate chipua,
Mamlaka kuyagawa,
Washike Watanzania.
676.
Hapo watakaobakia,
Si rushwa waliotoa,
Ila wanaojijua,
Na wajibu kutimia.
677.
Umaskini uchafu,
Unayo mbaya harufu,
Hili kujitaarifu,
Wote tukalikataa.
678.
Kuna wanaotumia,
Kuyapata manufaa,
Hao ni kuwashushua,
Akili zikarejea.
679.
Ziengwe rasilimali,
Kutufaa bilkuli,
Sasa kwa ilivyo hali,
Ufisadi umejaa.
680.
Juu walojikweza,
Wataka kuzimaliza,
Wawa kama waigiza,
Ila wanatuchuuza.
681.
Mikataba waridhia,
Kama vile ya kijuha,
Au wananunuliwa,
Psina sisi kujua.
682.
Sasa kinachotakiwa,
Tamko leltu kutoa,
Rasilimali ni dia,
Tunazimiliki raia.
683.
Pale kwetu tukivua,
Hiyo ni yetu ngekewa,
Mola katubarikia,
Japo hatukulijua.
684.
Iwepo asilimia,
Daima ya kuachiwa,
Kisha ndiyo kugaiwa,
Kitaifa Tanzania.
685.
Thamani kuichungua,
Iwe ni yetu tabia,
Na huo mtaji ukawa,
Kwa wazawa walokuwa.
686.
Waweza kujiuzia,
Au hisa kuridhia,
Umiliki wakajua,
Hali wanajinyanyua.
687.
Kijiji kikiamua,
Ubia kitawania,
Yao wakajifanyia,
Kisha wakajichomoa.
688.
kubwa wanayofanza,
Imani wanaikwaza,
Twaona wanajikweza,
Pekee wakajaliwa.
689.
Wao wakishapatiwa,
Sisti husahauliwa,
Mshirika wao kuwa,
Mwekezaji Tanzania.
690.
Tunaona wanapwaya,
Urahisi wanajitia,
Kidogo wanachochukua,
Mbona twaweza chimbua?
691.
Wanatakiwa kukua,
Njaa kuacha ugua,
Ili wapate tambua,
Ufakiri si laana.
692.
Wote tukijigawia,
Wala hautapungua,
Na kichowazuzua,
Kaburi wakimbilia.
693.
Yatayokujakutokea,
Mazuri hayatakuwa,
Salama hapatakuwa,
Ila maisha kuvia.
694.
Vipaji vya tasnia,
Katiba inatakiwa,
Muongozo kuutoa,
Kwa haki vikalelewa.
695.
Sasa yanayotokea,
Mmoja mmoja kuwa,
Mwenyewe akiamua,
Nani kumsaidia.
696.
Mifumo kuandaliwa,
Wote wakashughulikiwa,
Na zikawepo sheria,
Hili kuliangalia.
697.
Watoto wa Tanzania,
Haki sawa watakiwa,
Pasiwe kupendelea,
Na wengine kuonewa.
698.
Vijana wa Tanzania,
Fursa sawa kupewa,
Sio kwa vitendo na nia,
Ila kwa kazi kufanziwa.
699.
Wazee wanatakiwa,
Baraza wakaundiwa,
Wala sio kutumiwa,
Kama vile kitambaa.
700.
Kama vile kitambaa,
Mikono kujifutia,
Ila wakatunukiwa,
Nchi kuizungumzia.
701.
Nchi kuizungmzia,
Pasina kuegemea,
Na kama ni kuamua,
Haki ikawatangulia.
702.
Yao pia kwangalia,
Nafuu kujipatia,
Leo wasahauiwa,
kila mtu anajua.
703.
Twaweza kuwafufua,
Mchango bora kutoa,
Nchi ikatengamaa,
Na imara kwenda kuwa.
704.
Wazee wamejaliwa,
Umri walioukaa,
Maisha wanayajua,
Na vituko kung'amua.
705.
Wasipokuwa na njaa,
Huingia ushujaa,
Udhia wakakataa,
Halali kupigania.
706.
Ndivyo inavyotakiwa,
Mchango bora kutoa,
Nchi ikaendelea,
Kwa aali nadharia.
707.
Kinamama Tanzania,,
Makubwa wangetufanyia,
Wenyewe wangejijua,
Wala sio kutumiwa.
708.
Taasisi yatakiwa,
Kufunzwa sosholojia,
Pia na saikolojia,
Waweze kujikomboa.
709.
Kisha wakaongezewa,
Uongozi kuujua,
Na fitina wakatoa,
Wenyewe kujipendelea.
710.
Wajanja wakizaliwa,
Watu hutaka nunua,
Bei wakajipangia,
Ili yao kutimia.
711.
Husahau yakujua,
Hadi wakaulizia,
Hususan inapokuwa,
Magogo wanawekewa.
712.
Upande wanaujua,
Sana uliolegea,
Hukohuko huingia,
Vibeti kuvibetua.
713.
Sasa nchi yatakiwa,
Wananchi kuamua,
Si kugeuzwa majuha,
Mambo wakalazimishwa.
714.
Vikundi kuzinduliwa,
Jamii ikavitumia,
Yao kuyapigania,
Pasina kuingiliwa.
715.
Mgao ukitokea,
Watu wanaonunua,
Na wanaokataa,
Wao kutonunuliwa.
716.
Kuuzwa wanaokataa,
Sauti pia kusikiwa,
Sio tu mkawafaa,
Wanaotaka nunua.
717.
Ustawi wa jamii,
Kama hai silijui,
Naona haina uhai,
Kwa yanayoendelea.
718.
Juhudi zinatakiwa,
Idara kuiangalia,
Hapo ilipotiwa,
Naona inazidiwa.
719.
Idara ingelikuwa,
Mamlaka Tanzania,
Kaziye kuangalia,
Wanyonge waliokuwa.
720.
Kinamama walofiwa,
Na waume nao pia,
Mayatima Tanzania,
Uyatima wakomaa.
721.
Nani wa kuwaangalia,
Ila wa kuwahurumia,
Katika inatakiwa,
Hili likatatuliwa.
722.
Tunazo rasilimali,
Zinaosha kulhali,
Kushindwa uanzali,
Au utu watuishia.
723.
Hili pia laendana,
Na wa mitaani wana,
Walikuwa wachache jana,
Hivi leo ni mamia.
724.
Tutakuja pata laana,
Hili tusipolisana,
Yetu tukaharibiana,
Kwa hawa kuwaambaa.
725.
Watakuja changanyikana,
Wakashidnwa elewana,
Hepu wakaanza pambana,
Dhiki zikawanukia.
726.
Mifumo tumeishiwa,
Wala wengi hawajawa,
Ari tungelijaliwa,
Haya yasingetokea.
727.
Vijana twawaachia,
Paka tukawatishia,
Hofu zikiwaishia,
Tuna letu nawambia.
728.
Sasa kinachotakiwa,
Ni miundo kuzindua,
Na mifumo kufumua,
Upya tukajishonea.
729.
Hatuwezi tukalia,
Ajira zinapotea,
Na matatizo twajua,
Kedekese yamejaa.
730.
Matatizo Tanzania,
Fursa yaweza kuwa,
Vijana wakielewa,
Ajira kwao ikawa.
731.
Nyumba hatujajaliwa,
Na kiasi zapugnua,
Vijijini ni balaa,
Si nyumba viota huwa.
732.
Viwanda tukianzia,
Mbali mbali vyatakiwa,
Si wote moja kuzaa,,
Uzalshaji kugawa.
732.
Mikoa kuchaguliwa,
Viwanda -mbao kuwa,
Ubora wakishakuwa,
Dunia kuwanunua.
733.
Vya vyuma vinatakiwa,
Mali ghafi kuzitoa,
Wengine wakanunua,
Yao kujitengezea.
734.
Na vyakula navyo pia,
Viwanda vyake vyafaa,
Pahala tukachagua,
Rahisi panapokuwa.
735.
Aidha vinywaji pia,
Mikoa tungechagua,
Hyo ikatuzalishia,
Tusambaze TanZania.
736.
Saruji nayo mbolea,
Hivyo hivyo kuvigawa,
Pamoja vinapokaa,
Gharama zinapungua.
737.
Kilimo tukiamua,
Kitaajiri mamia,
Mtadi tukijitoa,
Kimasomaso ikawa.
738.
Msingi wakipatiwa,
Na chakula kugawia,
Wapo wataoridhia,
Kwenda kujitegemea.
Na uvuvi nako pia,
idha na kujifugia,
Na viwanda kuvizua,
Vya msingi kuzalisha.
739.
Vijijini nawambia,
Kwingine kwanistua,
Milioni wakipewa,
Wanaweza kujitoa.
740.
Wanaweza kujitoa,
Uongozi wakipewa,
Haya unayoyajua,
Njia ukawaonyesha.
741.
Taasisi zimezuka,
Huko hazijawahi fika,
Elfu kumi zinataka,
Zikaweza kukomboa.
742.
Benki kuu ikitaka,
Mayai inayoweka,
Ikatamia hakika,
Nchi juu itapaa.
Pesa kidogo ni dawa,
Mtizo kuondoa,
Masikini walokuwa,
Utajiri kunukia.
743.
Labda upo mwongozo,
Ulifanyalo mzozo,
Waogopa wenye nazo,
Umaskini ukiisha?
744.
Minong'ono yajaa,
Mtaji uliozuliwa,
Ni umasikini kulea,
Kutawala Tanzania.
745.
Makabila Tanzania,
Urithi tulojaliwa,
Uhaini kuyaua,
Kwa lolote lilokuwa.
746.
Umoja tumejaliwa,
Twajivuna Tanzania,
Na kitakachoundoa,
Ufisadi si kabila.
747.
Matabaka yataua,
Si ukabila wa lugha,
Umoja tuliouzua,
Mbali wakajitupia.
748.
Rushwa itauondoa,
Si makabila Tanzania,
Kwa jinsi inavyoenea,
Na watu kuivumilia.
749.
Makabila kuenziwa,
Iwe ni yetu tabia,
Makumbusho yakapewa,
Kuhifadhi historia.
750.
Na kwayo teknolojia,
Lugha zikahifadhiwa,
Nani anayeyajua,
Mbele vitatusadiia?
751.
Kawaida ni sheria,
Kwa watu wasiojua,
Udini ukitumiwa,
Hili kuondoa baa!
752.
Wapo wanaojizuzua,
Kawaida kuiua,
Budi kushughulikiwa,
Ndiyo haki ilokuwa.
753.
Mapya tukillia,
Na vitisho kutmia,
Wajinga waliokuwa,
Wataona wasikiwa.
754.
Watazidi kuroroma,
Na kuzizusha nakama.
Pakawepo uhasama,
Wa kijinga Tanzania.
755.
Mfano hili la kuchinja,
Wajua kina Masanja,
Dini moja walichinja,
Na wote tukaridhia.
756.
Ugumu halijakuwa,
Kuliko vita kuzua,
Serikali kuamua,
Kafiri kuruhusiwa.
757.
Ila tangazo kutoa,
Hakuchinjwa kauiwa,
Mnyama aliyekuwa,
Si halali kununua.
758.
Mabucha tukayatenga,
Yao yakatabandanga,
Na halali kuyakinga,
Yasije kuchafuliwa.
759.
Kuna wana Tanzania,
Wembe sasa walilia,
Kwa moja kuligundua,
Wadhani yote wajua.
760.
Kazi tukijipangia,
Na ufanisi zikawa,
Ufanifu nao pia,
Budi kuuangalia.
761.
Idadi ikizidia,
Kazi tunaichafua,
Kiasi inatakiwa,
Kutosha ni maridhia.
762.
Kisha wanaozipewa,
Kazi zao wakajua,
Sio kutunukiwa,
Madudu yatatujaa.
763.
Wajuzi waliokuwa,
Kazi zao kuachiwa,
Siasa zikiingilia,
Taifa hukorofisha.
764
Ujira kuangalia,
Riziki ikatimia,
Kila inapopungua,
Uovu mpya huzua.
765.
Masoko yanatakiwa,
Kwa wakuu kuyajua,
Wasiishie tembea,
Pasina cha kujiuzia.
766.
Balozi zingetakiwa,
Rasimu kuiandaa,
Kila nchi tukajua,
Nini cha kujiuzia.
767.
Nini cha kujiuzia,
Na rahisi kununua,
Wasiishi na kukaa,
kama vile matajiri.
768.
Hujisahau balozi,
Nchi wakawa hawawazi,
Wakaishia usingizi,
Na tija usiokuwa.
769.
Kufunzwa wanatakiwa,
Ujasiramali tabia,
Kazini kuutumia,
Wakistaafu pia.
770.
Bila hivyo hufulia,
Mengi yakawakimbia,
Na nchi kujikondea,
Minofu ikififia.
771.
Mawasiliano twajua,
Watu yanasaidia,
Na kilichobakia,
Unyonyaji kupungua.
772.
Hela zikichukuliwa,
Na wachache walokuwa,
kawaida inakuwa,
Ni vibaya kutumiwa.
773.
Vocha bei kupungua,
Na muda kuongezewa,
kiasi kitabakia,
Mengine kujifanyia.
774.
Dijito teknolojia,
Jinsi ninavyoelewa,
Urahisi yatakiwa,
Maisha kutufanyia.
775.
Ujanja ukipungua,
Gharama haitakuwa,
Mbadala kujaliwa,
Kawaida kurejea.
776.
Ila tukiwaachia,
Wajanja waliokuwa,
Pasina kuwa sheria,
Hili kuliangalia.
777.
Kwa miaka kama mia,
Mlaji kumrarua,
Hii ndiyo dunia,
Mabepari twawajua.
778.
Kompyuta Tanzania,
Budi kujitengezea,
Zetu zilizokuwa,
Kiswahili zatumia.
779.
Ni lugha iliyokuwa,
Kila mtu atumia,
Mwanzo wameanzia,
Wenye simu twasifia.
780.
Sasa ni kufatia,
Kompyuta kutumia,
Na mtandao ukawa,
Kiswahili kidedea!
781.
Vizuri tukijitoa,
Vyuo tutavifungua,
Kwa tovuti kutumia,
Afrika kuenea.
782.
Na ajira zikajaa,
Afika kufunzia,
Kiswahili kikakua,
Na uchumi kuinua.
783.
Nacho tusichojaliwa,
Viongozi wakujua,
Njia wanaotambua,
Wapi pa kuelekea.
784.
Vijiji kubwa hazina,
Kuvitunza vikafana,
Tena pasina hiyana,
Kwani tumevionea.
785.
Huduma nyingi zavia,
Kila mtu anajua,
Muongo unatakiwa,
Haya tuawapatia.
786.
Maji kutiririka,
Vijijini tunataka,
Waache kuhangaika,
Kinamama kuadhirika.
787.
Umeme kutochelewa,
Nyuma ukayafatia,
Gizani hatukuumbiwa,
Ni nani asiyejua.
788.
Nyumba nimeongelea,
Zastahili familia,
Kwa mbinu kujengewa,
Na ajira zikatoa.
790.
Hayo yakishakuwa,
Ndege yetu itapaa,
Mengine kuangalia,
Hali bora kufikia.
791.
Takwimu za Tanzania,
Watu shaka watilia,
Katiba ingetwakiwa,
Na hili kuliondoa.
792.
Ninachofikiria,
Mamlaka kuundiwa,
Na mtu isoingiliwa,
Kazi ikajifanzia.
793.
Kwa hivyo kuaminiwa,
Uhuru ikishajaliwa,
Jukumu ikalipewa,
Ukweli kupigania.
794.
Uongo kukaataa,
Na waongo kuumbua,
Mkuu hadhi akawa,
Katiba kumwangalia.
795.
Ya vyama yasiyofaa,
Hayo tutayaambaa,
Na ikulu ya kuzua,
Ukweli tukaujua.
796.
Ya tume yenye hadaa,
Yote tukayafichua,
Sensa bora kujaliwa,
Muongo kat ukiwa.
797.
Dawa tungejitambua,
Mbali tungeishakua,
Uizi uliingia,
Hakuna wa kuaminiwa.
798.
Katiba inatakiwa,
Wa jadi kuangalia,
Na msaada kupewa,
Vyao wakajiundia.
799.
Za asili tungetoa,
Na za kisasa kuzua,
Kama Wachina tukawa,
Uchumi tukajaliwa.
Subscribe to:
Posts (Atom)