MTANZANIA wewe ndiye unayemwajiri rais, mawaziri, wabunge na watumishi wa
umma. Na wewe ndiye mmiliki wa Katiba. Na katiba ni mchakato wa wewe
kuwaambia watawala waliopo na wajao unataka utawaliwe vipi na wao. Je, kuna
mtu mwingine anayeweza kuwasilisha ipasavyo unachokitaka kiwe, matakwa yako,
matarajio yako maslahi yako na ndoto ya Tanzania uitakayo na ile ya wewe
mwenyewe unachotaka kuwa kama sio mwakilishi wako anayeguswa na
yanayokugusa?
Kwa kuwa maendeleo hayatoki juu bali yanatokea chini kwa wananchi. Na diwani,
wajumbe wa nyumba kumi, makatibu kata na viongozi wa serikali za mitaa ni watu
muhimu sana katika uongozi huu wa ngazi za chini, je, kuna mipango yoyote ya
kuhakikisha kwamba watu hawa, yaani, wewe diwani na wenzako mnapatiwa
elimu itakayowasaidia kufaulisha kazi zenu ?
Ni kichekesho katika dunia ya leo kuwa na diwani ambaye hajasomea lolote
kuhusu uchumi, menejimenti, biashara, nadharia za kodi, menejimenti ya muda,
saikolojia, sosholojia, menejimenti ya fedha, masoko au nunuauza, uzalishaji mali,
ujasriamali, misingi ya uhasibu, menejmenti ya rasilimali watu na mengineyo kama
hayo.
Na hili linatokea pamoja na jitihada za wanaharakati wa maumizi ya Kiswahili
kupondwa na viongozi wa awamu mbalimbali wa nchi hii.
Lakini kama tungelikuwa tunatoa elimu kwa lugha ya Kiswahili toka ngazi ya shule
za msingi hadi Chuo au Chuo Kikuu angalau kwa viongozi wa serikali za mitaa,
mashule na taasisi za umma basi viongozi wetu wangeliweza kuhitimu vyema tu
katika masomo hayo na kuitumikia watu na nchi yao kwa ufanisi na ufanifu wa hali
ya juu zaidi.
UTAFITI UNAONESHA KWAMBA ASILIMIA 94 YA WATANZANIA HAWAJAWAHI
KATIKA MAISHA YAO KUKUTANA NA MWINGEREZA, MFARANSA, MRENO,
MHISIPANIA, MCHINA, MJAPANI na kuzungumza naye kwa lugha nyingine
yoyote isipokuwa KISWAHILI.
Ni asilimia hiyo 94 ya Watanzania inayotuhoji pia kwanini tunakataa kuwafundisha
elimu na maarifa mapya kwa lugha mama yao Kiswahili.
Je, wakati haujafika wa kuwa na Taasisi iwe binafsi au ya umma ambayo itakuwa
ikitoa elimu ya chekechea, msingi, sekondari, chuo hadi chuo kikuu kwa kiswahili
katika masomo yote kama taasisi ya mfano na majaribio ili kutathmini kwa vitendo
na kufanya maamuzi sahihi kuhusu nafasi ya Kiswahili Tanzania, Afrika Mashariki
na duniani kwa ujumla ?
Diwani unawajibika kuingia katika Baraza la Katiba mpya ili kusaidia kuwa na
katiba ambayo pamoja na kushinikiza matumizi mapana na marefu ya Kiswahili
itachangia Watanzania wengi zaidi kuelimika na kuneemeka na lugha mama yao.
WATAKAOCHANGIA bila uchama, ukabila, ueneo, udini, ubinafsi na ushawishi wowote toka kundi lolote ndani au nje ya nchi watastahili kupewa tunzo ya juu kabisa ya Kitaifa.
NI haki na wajibu wenu pia kuwaamsha, kuwafundisha na kuwaelekeza wananchi wengine nini wanachopaswa kufanza ili mahitaji yao ya msingi, dhiki, mapungufu kwao, kasoro zilizopo kwenye maeneo na maisha yao, haki na maslahi yao yote yaweze kupatikana kwa kutumia katiba na sheria za nchi na sio vinginevyo.
Ni muhimu pia wananchi kuelewa kwamba serikali ni kitu kinachodumu milele mpaka mwisho wa dunia lakini vyama vya kisiasa ni taasisi za kupita, leo vinaweza kuwepo na kesho visiwepo na vikaja vyama vipya kabisa madarakani.
No comments:
Post a Comment