NCHI nyingi za Kiafrika zina kichekesho kimoja kikubwa. Kichekesho hicho sio
kingine ila ni kile cha wanasiasa (wengi wakiwa hawana hata nusu ya kisomo cha
madaktari) kulipwa mishahara mikubwa kuliko jeshi hili muhimu la kuokoa maisha
ya raia wetu.
Ndiyo maanake hata madaktari nao wanataka kuingia kwenye siasa ili
waondokane na mishahara njaa. Je, hivi kwa akili na upeo wetu daktari anastahili
kulipwa mshahara mdogo kuliko diwani,mbunge, waziri au hata dereva au
mtumishi wa ndani wa waziri kweli ? Na jamaa hawa wakitimkia nje hivi kweli kilio
chetu cha uzalendo kitasaidia kitu? Sio kwamba wakati umefika wa wabunge,
mawaziri kulipwa mshahara unaolingana na elimu, ujuzi na vyeti vyao? Badala ya
nafasi hizo kuwa za kwenda kujilimbikizia utajiri ziwe ni changamoto kwa wale
wanaotaka kuacha kazi zao au biashara zao kuingia kwenye siasa ? Na kwamba
hadi wa leo hatujapindua kichwa -chini na miguu-juu ssuala hili la mishahara. Kwa
maana ya kuwa sio wanasiasa waliostahili kulipwa mishahara mikubwa bali
washiriki moja kwa moja kwa vitendo kwenye sulubu na maumivu ya kuwajenga
Watanzania kiafya, kiakili na kimwili ili wachangie si haba pato la taifa na
maendeleo ya jamii zao na nchi yao?
Tanzania laiti ingelikuwa na mikoa huru kiuchumi na kijamii serikali za mikoa na
wakazi wa mikoa husika wana uwezo wa kuzifanya hospitali zetu kuwa bora kiasi
ambacho wagonjwa wengi katika nchi mbalimbali za Kiafrika wakaja hapa kutibiwa
na kuuguzwa badala ya kupelekwa nchi za nje ? Na hili likifanyika ni kwamba
mishahara, marupurupu yenu na kipato chenu kwa ujumla kitaongezeka na
hamtakuwa na sababu ya kukimbilia nchi za nje !
Jitayarisheni, jiandaeni na kujihami na nguvu za hoja kuhusu umuhimu wa kuwa
na Baraza au Mkutano wa Kitaifa wa Katiba Mpya 2011 na wala sio Tume au
Kikundi cha wateuliwa wachache hata kama ni mawaziri, wabunge, majaji,
wanasheria na engineo kama hao, maana historia inaonesha wote hao hawawezi
kutetea maslahi yako wewe na kwamba mwamba ngoma ngozi lazima
avutie kwake au sio?
NCHI inayowaheshimu madaktari na manesi wake na kuwa na vifaa vya kisasa vya tiba, wafanyakazi wachapakazi, mazingira mazuri kwa wafanyakazi na wagonjwa mahospitalini inaweza kupata fedha za kigeni kutokana na kuja kwa wagonjwa wengi kutoka nchi jirani na za mbali kutibiwa hapa kwetu.
No comments:
Post a Comment